Saturday, April 6, 2013

RIWAYA: PAINFUL TRUTH (UKWELI WENYE KUUMA)----------2


MTUNZI: Nyemo Chilongani

MAWASILIANO: 0718 06 92 69

SEHEMU YA PILI


Wayne akalala kifuani kwake, Happy akabaki akilia tu kwa maumivu makali. Bikira ambayo alikuwa nayo ndio ilikuwa siku ya mwisho kukaa mwilini mwake. Shuka likatapakaa damu. Happy akabaki akilia, hakuamini kama kweli kwa siku ile alikuwa amefanya mapenzi kwa mara ya kwanza.
“Mungu wangu! Kumbe niko kwenye tarehe zangu za kupata mimba” Happy alijisemea huku akionekana kushtuka katika kipindi ambacho Wayne akiwa pembeni akichukua taulo na kuelekea bafuni kuoga.



Macho ya Happy yakaanza kuwa mekundu, machozi yakaanza kujikusanya machoni mwake na baada ya sekunde kadhaa yakaanza kutiririka mashavuni mwake. Hakuamini kile ambacho kilikuwa kimetokea dakika chache zilizopita.
Alichokifanya huku akionekana kuchanganyikiwa ni kuanza kukimbia kuelekea nje ya chumba kile. Akaanza kushusha ngazi haraka haraka kuelekea chini huku akionekana kuchanganyikiwa.
Alipofika nje ya jengo la hoteli ile, akaanza kukimbia kuelekea nyumbani kwa shangazi yake. Njia nzima alikuwa akilia, moyoni alionekana kuumia kupita kawaida, kufanya mapenzi katika moja ya siku ambazo alikuwa na uhakika wa kupata mimba kulionekana kumuumiza kupita kawaida.
Alitumia dakika thelathini mpaka kufika nyumbani kwa shangazi yake, moja kwa moja akaingia chumbani na kujifungia. Hakutaka kutoka nje, aliamini kwamba kama angekaa ndani kwa muda mrefu basi angeweza kujisahaulisha na kile ambacho kilikuwa kimetokea.
Bi Selina akaonekana kumshangaa Happy, hakuelewa sababu ambayo ilimfanya kurudi nyumbani hapo huku akilia. Alichokifanya ni kuanza kumfuata chumbani kwake, alipoufikia mlango, akaanza kuugonga. Happy hakufungua mlango japokuwa alisikia fika kwamba Selina yake alikuwa akiugonga mlango ule.
Bi Selina aligonga mlango zaidi na zaidi, Happy akaamua kuufungua mlango. Selina akaanza kumfuatta happy pale kitandani alipokuwa na kisha kukaa pembeni yake. Kila alipojaribu kumuuliza, Happy hakujibu chochote kile zaidi ya kuendelea kulia.
“Tatizo nini Happy?” Bi Selina aliendelea kuuliza lakini Happy hakujibu kitu zaidi ya kuendelea kulia.
Bi Selina aliendelea kumbembeleza Happy zaidi na zaidi lakini Happy hakujibu kitu chochote kile. Alichokifanya Bi Selina mara baada ya kuona kwamba Happy haongei kitu chochote kile, akaamua kuondoka ndani ya chumba kile.
Happy hakujua afanye nini, hakujua kama angetakiwa kumwambia shangazi yake au la. Aliendelea kubaki chumbani kwa dakika kadhaa, baada ya muda akashtukia shangazi yake akianza kupiga hodi tena.
Mara hii akaingia huku akiwa katika hali ya kawaida, kwa mbali alionekana kukasirika. Akamfuata happy pale kitandani na kisha kukaa karibu nae. Akamwangalia Happy katika mtazamo ambao ukaonekana kumtia wasiwasi.
“Mbona umemkimbia yule mzungu?” Bi Selina aliuliza.
Happy hakujibu chochote kile, swali lile ambalo alikuwa ameulizwa likaonekana kuanza kukivuta tena kilio chake na kisha kuanza kulia tena. Alikumbuka vilivyo sababu iliyompelekea kumkimbia Wayne ndani ya chumba kile.
“Mbona umemkimbia mwezako?” Bi Selina aliendelea kuuliza.
“Nimeamua” happy alijibu.
“Alikupa hizo hela?” Bi Selina aliuliza.
“Ndio”
“Sasa kwa nini umemkimbia?” Shangazi alirudia swali lake.
Happy akashindwa ajibu nini, hakujua kama kulikuwa na sababu ya kumwambia shangazi yake kile ambacho kilikuwa kimetokea hotelini au la. Akayapeleka macho yake usoni kwa shangazi yake, akaanza kuyafuta machozi yake.
“Yule mzungu anakusubiri nje” Bi Selina alimwambia.
Happy akaonekana kushtuka kupita kawaida, hakuamini kile ambacho alikuwa amekisikia kutoka kwa shangazi yake. Alipanga moyoni mwake kwamba hakutaka kuonana tena na Wayne, kitendo kile alichokifanya cha kufanya nae mapenzi kilionekana kuanza kumuwekea aibu moyoni mwake.
“Yupo nje anakusubiri” Shangazi yake alimwambia mara baada ya kuona amekaa kimya kwa sekunde kadhaa.
“Sitaki. Sitaki kuonana nae” Happy alijibu.
Bi Selina alionekana kutokuelewa kitu chochote kile. Hakujua sababu ambazo zilimfanya Happy kukataa kuonana na Wayne na wakati nia asubuhi tu walikuwa wameondoka wote. Akaanza kuona kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kimetokea ila Happy hakutaka kumwambia.
“Niambie kuna kitu kimetokea?” Bi Selina alimuuliza.
“Hapana”
“Sasa kwa nini hautaki kuonana nae?”
“Nimeamua tu” Happy alijibu.
Bi Selina hakutaka kuendelea kubaki chumbani mule, alichokifanya ni kutoka chumbani mule na kuelekea nje.
****
Muda wote Wayne alikuwa akifurahia, hakuamini kwamba katika maisha yake angeweza kupata msichana ambaye alikuwa bikira na kuitoa yeye mwenye. Bikira ambayo alikuwa ameitoa kwa happy ilionekana kumchanganya kupita kawaida, muda wote bafuni alikuwa akiimba kwa furaha tu.
Akatoka bafuni na kisha kurudi chumbani. Akaanza kuangalia huku na kule, Happy hakuwepo. Wayne akaonekana kuchanganyikiwa, hakuelewa ni kitu gani ambacho kilimfanya Happy kuondoka ndani ya chumba kile pasipo kumuaga. Alichokifanya ni kuvaa nguo zake haraka haraka na kisha kutoka chumbani mule na kuelekea alipokuwa akiishi Happy.
Ingawa alikuwa akipata shida katika kuzikumbuka njia lakini alifanikiwa kufika. Akamkuta Bi Selina akiwa nje akifua nguo. Akamsalimia na kisha kumuulizia Happy. Alimueleza kila kitu ila hakumueleza kama alikuwa amefanya nae mapenzi.
Bi Selina akaonekana kukasirika, alichokifanya ni kuingia ndani ili amuite Happy. Wayne alibaki nje huku akionekana kuwa na furaha. Kitu pekee ambacho alikuwa akitaka kukiona kwa wakati huo ni kumuona Happy kwa mara nyingine tena.
Japokuwa kilikuwa kimepita kipindi kifupi lakini moyo wake ukaonekana kumkumbuka Happy. Hakutaka kuondoka mahali hapo pasipo kumuona Happy. Moyo wake tayari ulikuwa umekwishatekwa na binti huyo kiasi ambacho akaanza kumsahau Kristen , mchumba wake aliyekuwa nchini Marekani.
Bi Selina akarudi mahali hapo, Wayne bado alikuwa mvumilivu kusubiri, alipopewa taarifa kwamba Happy alikataa kutoka nje, moyo wake ukanyong’onyea kupita kawaida.
“But I want to see her (Lakini ninataka kumuona)” Wayne alimwambia Bi Selina.
“I know. She cried a lot. What happened when you left here? (Ninafahamu. Alilia sana. Nini kilitokea mlipoondoka mahali hapa?)” Bi Selina aliuliza.
“Nothing. We had some soft drinks somewhere but unfortunately she ran away. I tried to come after her but she disappered from my presence (Hakuna kitu. Tulikuwa tukipata vinywaji sehemu fulani, ghafla akaanza kukimbia. Nilijaribu kumfuatilia lakini akapotea katika uwepo wangu)” Wayne alimwambia Bi Selina.
“Ok! Dont worry. Just give me time, I will talk to her and tell you what happened to her (Sawa! Usijali. Nipe muda niongee nae na nitakuambia nini kilitokea)” Bi Selina alimwambia Wayne.
Wayne hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuanza kuondoka kurudi hotelini. Njia nzima alikuwa na mawazo, hakuamini kile ambacho kilikuwa kimetokea. Lengo lake kubwa lilikuwa ni kumuona Happy kwa mara nyingine kwa sababu alikuwa amemkumbuka sana, lakini mwisho wa siku alikuwa akirudi hotelini bila kuonana nae.
Akaingia ndani ya chumba kile na kisha kulala. Kwa wakati huo, Happy ndiye ambaye alikuwa amekitawala kichwa chake. Alimkumbuka sana Happy hata zaidi ya alivyokuwa akimkumbuka mpenzi wake aliyemuacha nchini Marekani, Kristen.
Simu yake ya mkononi ambayo ilikuwa imeunganishwa na mtandao wa kimataifa wa Tricom ikaanza kuita. Akainuka kivivu kitandani pale na kisha kuinyanyua simu ile kutoka mezani. Akakibonyeza kitufe cha kijani na kuanza kuongea.
“Rudi haraka sana nyumbani” Sauti ya upande wa pili ilisikika.
“Kuna nini baba?”
“Kuna tatizo. Kristen amezidiwa. Ugonjwa wa pumu umemuanza tena” Sauti ya baba yake ilisikika.
“Unasemaje! Sawa, nitakuja huko haraka iwezekanavyo” Wayne allijibu.
Tayari akaonekana kuchanganyikiwa, taarifa ambayo alikuwa amepewa ikaonekana kumchanganya kupita kawaida. Taarifa za kuumwa kwa mchumba wake zikaonekana kumshtua kupita kawaida. Mawazo juu ya Happy yakafutika na kuanza kumfikiria Kristen.
Ni kweli alikuwa akimpenda sana mchumba wake huyo japokuwa katika masaa machache yaliyopita alikuwa amemsaliti kwa kufanya mapenzi na Happy. Kristen hakuwa katika hali nzuri, mara kwa mara ugonjwa wa pumu ulikuwa ukimsumbua kupita kawaida.
Aliona kulikuwa na kila sababu za kusafiri na kurudi nchini Marekani kwa ajili ya kumuona mpenzi wake. Alihitaji kukaa na mpenzi wake na kumuonyesha kwamba alikuwa akiendelea kumthamini japokuwa alikuwa na ugonjwa huo ambao ulikuwa umemtesa kwa kipindi kirefu.
Akapanga mipango ya safari, alitakiwa kurudi nchini Marekani haraka iwezekanavyo. Siku iliyofuata, akawa ndani ya ndege akirudi nchini Marekani. Kichwa chake kimoja kiilikuwa kikiwafikiria watu wawili tu, Kristen na Happy.
“Nitachagua wa kumuoa hapo baadae. Ila hata Happy nae anafaa sana. Mmh! Wazazi watanielewa vipi kama nikimuoa? Kwanza hawamjui hata mara moja, wataweza kuniunga mkono katika maamuzi yangu? Mmh! Huo nao uamuzi mgumu” Wayne alijisemea wakati ndege ikiwa imekwishafika katika ardhi ya Morocco tayari kwa kuendelea na safari ya kuingia Ulaya na kisha kuelekea Marekani.

Je ni nini kitaendelea?
Je ni uamuzi upi ambao atauchagua Wayne?
Je Wayne ataamua kumuoa msichana Happy au Kristen?
Itaendelea.




No comments:

Post a Comment

Recent Posts