Saturday, April 6, 2013

RIWAYA: MREMBO ALIYEPOTEA---------------6

MTUNZI: Andrew Carlos


MAWASILIANO: 0713133633

 

SEHEMU YA SITA


Taratibu John akaanza kufungua jicho lake moja na baadaye likafuatia jngine na sasa akawa anaangaza huku na kule nakushangaa watu waliokuja kumuona.
“Mke wangu yuko wapi? Angel wangu yupo wapi nimesema?”
John alishtuka nakuanza kumtaja Angel hali iliowafanya kila mmoja wa marafiki zake kumshangaa hadi mkewe wakajua atakuwa amechanganyikiwa na kukosea kwa kumtaja Angel badala ya mkewe Janet. Akili ya Janet sasa ikawa ni kuhakikisha mumewe anajua kuwa yupo pale nakuwa amrekebishe mumewe asimtaje Angel amtaje Janet.
“Mume wangu?, nimekuja ni mimi Mkeo Janet, amka ule?”
“Hapana najua wewe ni Janet lakini namtaka Angel wangu sasa hivi”
“Angel ndio nani?, kwanza Angel hayupo hapa yupo kwao hukoo!”
Janet alijikaza bila ya kujua angel anayezungumziwa na John hivyo akaona kama amemdanganya atatulia tu.
“Jamani sitaki mivyakula yenu namtaka Angel nimesema?, Kwanza Alice nayeye amepona? yupo wapi?”
Hasira kali zilizoambatana na wivu ndani yake zikaanza kujijenga kichwani mwa Janet, Ule uvumilivu aliokuwa ameuonesha toka mwanzo ukawa sasa umeisha. Akaona dunia chungu kwa muda, Hakuamini kama mumewe John yupo siriazi kwa kutaja hao wanawake asiyewajua hata kwa sura. Akafikiria mengi sana mpaka akajiona hana thamani hata kwa mwanaume yeyote, aliamini kila rafiki yake aliyekuja kumtembelea atakuwa anajua matatizo yake ya kutokuzaa hivyo hata hao anaowataja John watakuwa wanamjua ila wanamficha tu. Akaamua kujishusha kama mwanamke aliyefundishwa na wazazi nakuanza kumbembeleza John ale kwa mara nyingine.
“Mume wangu John!, kula basi halafu ndio uongee hayo mambo mengine!”
“Hivi hamnisikii heee, wewe nimesema sikutaki tena maishani mwangu, na ni mmoja tu aliokuwa amebeba mimba yangu na nilimpenda sana, Angel!! Yes! Angel!! nipelekeni nikamuone”
John hasira zilimpanda zaidi akachukuwa bakuli ambalo tayari Janet alikuwa amemimina zile ndizi na kumwaga chini, Kisha akajitoa ile dripu aliokuwa amefungwa nakuinuka.
“Haya namtaka Angel wangu sasa hivi?, Na pia nataka nimuone Alice?”
Ule uvumilivu ambao ulikuwa ukioneshwa na marafiki zake na John na hata wafanyakazi wenzake sasa ukawa umefika ukingoni. Wakajitahidi sana kumvumilia nakumuona kama mgonjwa, ikawabidi waingilie kati ugomvi ule aliokuwa ameuanzisha John mule wodini.
“Hivi John rafiki yetu? uko sahihi kweli kwa unachokinena mbele ya mkeo. hivi unajua thamani yake wewe? Si mkeo wa ndoa huyu”
“Hata kama mke wa ndoa jamani lakini siwezi nikaponeshwa hiki kidonda ambacho kimenitokea cha kuondokewa na Angel?”
“Angel? Angel ndio nani?, Maana sisi kama wafanyakazi wenzako tunamtambua Janet kama mkeo na hata kwenye nyaraka zote za kwako za ofisini zinamtambua mkeo kama mrithi wa vitu vyako japokuwa bado huna mtoto”
Akili ya john sasa ikawa kama imeanza kuelewa kitu gani anachosemeshwa, japo alinyanyuka alijikuta mwenyewe akirudi tena mpaka chini kukaa kitandani huku akichukuwa mkono wake na kumshika mkewe Janet. Alimuangalia mkewe kwa jicho la aibu na kukaa kimya kwa muda kisha.
“Nakupenda sana Mke wangu!!”
“Nakupenda pia Mume wangu!”
Mwili wa Janet ulijihisi kusisimka, Akamwangalia rafiki yake Mary waliokuja naye kwa tabasamu. Akaifananisha siku hii kama ile siku yake ya ndoa walipokuwa wakifungishwa kanisani na mchungaji. Kitendo cha kuchukuwa chombo kingine na kumuwekea tena uji mumewe alifananisha na tukio la kuchukuwa pete na kumvalisha John. Moyo wa Janet haukuwa tayari kuvunjika haswa kwa mtu ambaye hata hamfahamu. Jina la Angel sasa likawa limemfutika John ghafla. Akajihisi kuwa na ganzi ya mwili kwa muda, kila akinyoosha shingo yake kuwaona wageni waliomtembelea ndipo na akili yake ikawa inafanya kazi vizuri.
“Haya kunywa basi mume wangu?”
“Sawa nipe taratibu tu”
John alikubali kupokea vijiko vya uji kutoka kwa mkewe Janet nakunywa. Hakuwa mbishi tena kama alivyokuwa hapo awali. Kila mmoja aliyekuja hapo kumtembelea alikuwa na sura ya tabasamu kuona John akiwa katika hali ya furaha na amani kwa mkewe. Alipomaliza kunywa uji tu, bosi wake aliyekuwepo pembeni akamkabidhi bahasha ya kaki iliyokuwa na kiasi kidogo cha pesa ndani yake kisha akamuaga. Muda wote Mary jirani yake na Janet alikuwa pembeni akimsubiria Janet waondoke lakini haikuwezekana kuongozana naye tena.
“Janet?, wacha na mimi niwahi nyumbani kupika si unajua sijaandaa chochote na watoto niliwaacha wameenda shule”
“Haya mimi acha niwe karibu na mgonjwa wangu, tutaonana huko huko nyumbani shosti”
“Haya baadaye, shemeji?”
“Naam!!”
“Ugua pole shemeji wangu nitakuja kukuona jioni au kesho asubuhi sana!”
“Ok ahsante kwa kuja”
Watu karibu wote walikuwa wameshaondoka, na sasa John alibaki kitandani na mkewe pembeni huku akimfariji. John alijihisi ni dhambi nyingi sana anazo kwa kumtendea mke wake katika kipindi cha nyuma. Wazo la kumng’ang’ania Angel na kumtaja ovyo akaliyeyusha ghafla. Ni kama aliendewa kwa mganga kwa muda maana alivyomsahau ghafla hata hakutaka kuamini. Alijipa moyo na kuhaidi kuendelea kuwa na mkewe milele.
“Sasa Alice atahudumiwa na nani? ndio inabidi niachane na Angel kwanza ameshafariki lakini nitakuwa na dhambi endapo nitamtelekeza na Alice.. Hapana hapa haiwezekani?”
John alijikuta akiusemea moyo huku akimfikiria sana Alice. Alikuwa katika dimbwi kubwa la mawazo, Alishinda kabisa jinsi ya kumuanza mkewe juu ya Alice kwani ni lazima angemtaja Angel ambaye walizua ugomvi muda mfupi uliopita. Alijitahidi kujikaza na kuvumilia mpaka muda ambao daktari alikuwa akiwapitia na kuwajulia hali ndipo John akanyanyua kinywa chake na kuuliza.
“Samahani daktari?”
“Bila samahani mgonjwa uliza tu?”
“Jana nilikuwa naamuulizia yule mgonjwa wa kike niliyekuja naye usiku wa jana”
“Annhaa, ndio wewe kumbe?”
“Ndio mimi dokta!!”
“Yule binti kajitahidi kutuelekeza lakini tumeshindwa kukufahamu vizuri kama ni wewe ndio uliokuwa na yule. Kwa maana mlipokelewa na manesi wa zamu wengine ambao kwa sasa hawajafika mpaka usiku ndio zamu yao ikabidi tusubiri wakija hiyo usiku ndipo waweze kukutambua.. Aisee umefanya jambo la busara sana. Sasa!!,”
“Ndio dokta”
“Kwa sababu yule binti hakuwa na tatizo sana zaidi ya kuishiwa pumzi hivyo mpaka kufikia alfajiri hali yake ilikuwa safi na alikuwa akipumua vizuri tu na kwa sasa tumemuacha apumzike tu huku akisubuiri ndugu zake waje kumchukuwa.”
“Ndugu zake ndio sisi dokta?”
John alijibu kwa haraka haraka hali iliyomfanya Janet kutokuelewa kitu na kuona kama John ameanza tena kuchanganyikiwa kama hapo awali alivyokuwa akifanya. Kitendo cha kusema ni ndugu yao wakati hata kwa sura Janet hamfahamu huyo binti anayezungumziwa ilikuwa ni fumbo kubwa sana kwa Janet.
“Ngoja nikamchukuwe nakumleta sasa hivi!!, wala msiwe na shaka”
Yale maneno ya dokta yalimfanya Janet amuangalie mumewe John kwa jicho la ukali na hasira ya hali ya juu, Japokuwa walibaki wawili tu pale kitandani lakini tayari wivu ulikuwa umekizunguka kichwa na mwili wake kwa ujumla, Janet alikuwa na wivu sana katika suala zima la mapenzi. Alijua ni wazi watakuwa ni visichana vyake ambavyo John hutembea navyo pindi amelewa hivyo mara ya mwisho watakuwa walikuwa wote wakinywa na mpaka wakapata ajali. Hakutaka kuropoka wala kufanya ugomvi lakini duku duku ambalo lilimkaa moyoni alikuwa akitaka kulitoa..
“John Mume wangu?”
“Eenhee niambie mpenzi”
“Samahani lakini mume wangu kma nitakuwa nimekukosea”
“Bila samahani niambie tu mke wangu”
“Eti?, huyo binti aliyeenda kuletwa na daktari ni nani kwako?”
Janet alionesha kujiamini kwa kumuuliza John huku akimtolea macho kwa msisitizo akitaka ajibiwe juu ya huyo binti. Kwa kujiamanini John alimuelezea vyote kuhusiana na mchezo mzima aliokuwa akiufanya juu ya Angel mpaka alipokuja kujuana na Alice ambaye ndiye mdogo wake na marehemu Angel. Janet alisikitika sana kwa mimba ambayo alikufa nayo Angel. Aliona mumewe anamakosa sana lakini akaapa kutoka moyoni mwake kuwa amemsamehe na kuahidiana kamwe haitakuja kutokea tena kitendo kama hicho cha aibu. Sasa Janet ana John wakarudi kama zamani kama mke na Mume waliokamilika na kwa muda huu walikuwa pamoja huku John ameegemea katika kitanda cha wagonjwa wakimsubiria Alice ambaye alienda kuchukuliwa na daktari. Muda wa dakika takribani kumi zilimtosha dokta kwenda na kurudi na Alice, hakuwa amevaa mavazi yake ya jana yake usiku sababu yalilowa sana na damu hivyo alikuwa amevalishwa mavazi spesho ya hospitali na sasa alkuwa ameshikwa mkono na dokta huku wakikaribia eneo ambalo alikuwepo John na mkewe.
“Alice!! hujambo? ”
“Sijambo kaka shikamoo!!, Shikamoo dada”
“Marhaba!!, Vipi unajisikiaje?”
“Hapana sina tatizo tena kaka, najisikia vizuri tu”
Alice alijibu kwa uoga huku akimtolea macho mke wake John bila ya kumfahamu kama ni mke wa John au la!. John Alimpokea vizuri Alice na kisha dokta yule akaondoka hivyo wakabaki watatu. Kikao kifupi ambacho John alikitengeneza cha yeye mkewe na Alice kilikuwa jibu tosha kwa Janet kumfahamu Alice. Alimsikitikia sana na kuahidi watakuwa pamoja katika kumsaidia Alice. Japo Alice alikuwa bado katika majonzi ya kuondokewa dada yake lakini Alice alijiona tena mwenye bahati ya mtende baada ya Janet na John kuafikiana kumsaidia Alice kwa hali na mali mpaka mwisho wa maisha yake.

****

Muda wa mwezi ukawa umekatika kwa Alice kumsahau dada yake Angel. Kwakuwa Angel hakuwa na ndugu yeyote Dar es salaam na wala hakukuwa na mtu aliyepafahamu nyumbani kwao Kigoma hivyo ikabidi azikwe chini ya manispaa na zoezi hilo lilifanyika kwa haraka nakuhuduriwa na Alice, Janet na John tu. Alice alijitahidi kusahau lakini ilikuwa ni vigumu kidogo. Mali zote ambazo Angel alikuwa nazo zikawa chini ya Alice. Ni John pekee ndio alitoa wazo la kuziondoa mali zote nakuzihamishia kwake na pia kuishi na Alice kwakuwa alikuwa ndio kwanza ana miaka kumi na nane na hakuweza kujitegemea mpaka angekuwa na mtu au anafanyakazi. Wazo hilo lilipokelewa na Alice bila kizuizi chochote na sasa akawa chini ya familia ya John na mkewe Janet. Furaha yake ya maisha ikarudi pale pale kwa kuwa janet hakuwa na uwezo wa kuzaa hivyo alimchukulia Alice kama mtoto wake wa kumzaaa. Elimu yake ya darasa la saba aliyosomesha na baba yake miaka ya nyuma haikukidhi kabisa kuelewana na mtu yeyote msomi. Hivyo John alikuwa bega kwa bega katika kumsaidia Alice na kitu alichokifanya ni kumpeleka kozi ya kiingereza kisha akampeleka kujifunza kompyuta. Sasa Alice akawa siyo Alice yule wa zamani. Uzuri wake ukaongezeka maradufu. Aliijiheshimu sana mbele ya John na Janet kwakuwa aliwachukulia kama wazazi wake wa kumzaa. Kazi aliyokuwa akiifanya John ya kusimamia walimbwende wa Tanzania sasa ikawa imehamia kwa Alice. John alitaka Alice ashiriki mashindano hayo.
“Alice mwanangu?, nahitaji ushiriki katika miss Tanzania mwaka huu?”
“Kweli dady?”
“Ndio kwani nakuona kwa sasa unafaa na unaweza kushinda na ukafika mbali sana tu”
“ I love you dady wangu!!”
“Hivi ukiwa kama mrembo anayeiwakilisha Tanzania mwanangu vitu gani utavifanya?”
“Kwanza kabisa kama shughuli ambazo huwa zinateuliwa za kusaidia jamii, nitahakikisha nimeisaidia jamii yangu kwa asilimia kubwa tu na malengo yangu haswa ni kusaidia wanawake wasiojiweza hapa namaanisha vikongwe. Ujue nini baba? serikali yetu inawasahau sana hawa watu sasa mimi nitakuwa bega kwa bega kuhakikisha wanapata huduma zinazostahili”
John alibaki akitikisa kichwa akishangaa kwa maneno ambayo Alice akiongea, hakuamini kama Alice huyu anayemjua ndio anaongea ama ameambiwa na mtu mwingine. Ikambidi amtege tena.
“Eenhee!!! mwanangu na kitu gani kingine utakifanya ukiwa kama mrembo anayewakilisha hapa Tanzania??’
“Natamani sana kuwasaidia vijana wenzangu ambao wamepoteza mwelekeo wa kimaisha, hapa naamaanisha kwa wakiume na wakike. Kuna dada ambao wameshakata tamaa ya kuishi na hata wengine wameishia kujiuza miili yao na wengine kuhamia kwenye madawa ya kulevya. Ujue baba sisi wanawake ndio tunaonewa na kunyanyaswa sana haswa tunapoingia katika suala zima la ndoa, wanawake tumekuwa hatuthaminiwi nakupewa haki zetu za msingi hivyo basi nikiwa kama mrembo atakayeiwakilisha Tanzania nitahakikisha nakuwa sambamba na taasisi ambazo zinajishughulisha na masuala haya ya kusaidia wanawake ili kuweza kutokomeza tatizo zima la kunyanyaswa. Na kuhusu wanaume napo vijana wenzangu wengi sana wamepotea haswa kwa kufuata mikumbo wanajikuta mwisho wa siku wana ingia katika biashara za kuuza madawa na hata wengine kuyatumia na mwishowe kuwa mateja na hata kupoteza nguvu ya taifa”
John sasa akawa ameshusha pumzi zake kwa maneno ya ushawishi ambayo alikuwa akiyatoa Alice. Hakutaka kuamini hata kidogo kama aliyekuwa akizungumza naye ni Alice kweli ama mwingine lakini ikabidi aamini ukweli aliokuwa akiushuhudia mbele ya macho yake.
“Sasa mwanangu si unajua mashindano haya huwa yanaanzia ngazi za mikoa lakini kwa hapa Dar yamegawanyika kwa wilaya hivyo kuna mkuu mwenzangu anasimamia kanda ya Chang’ombe na wewe ndipo utakapoenda kugombea huko, haina wasiwasi kuhusu ushindi kila kitu tutaweka sawa cha msingi onesha kujiamini tu mwanangu”
“Sawa baba nakuhaidi sintokuangusha, Wewe mwenyewe utajionea, naweza dady niamini kwa hilo, naweza na tena napenda sana”
John alionesha tabasamu kwa kukubaliana na Alice. Kuanzia sura umbo na hata muondoko ulimthibitishia kuwa Alice anafaa kujiunga na mashindano hayo. Siku nzima ikawa ni furaha sana kwa Alice, alijihisi ndoto zake za miaka ya nyuma juu ya maisha yake sasa zinaenda kufanikiwa. Alijihakikishia Tanzania nzima na dunia kwa ujumla iweze kumtambua mchango wake na kumjua yeye ni nani katika jamii. Hata Janet mke wa John alihafiki kitendo cha Alice kujiingiza rasmi katika mashindano ya kumtafuta mrembo wa Tanzania. Baraka zote alizopewa Alice zilizidi kumuweka katika hali tofauti. Alifanya kazi zote kwa bidii, hakutaka kamwe amuudhi Janet wala John katika maisha yake kwani ndio walikuwa walezi wake kwa sasa.

ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment

Recent Posts