Monday, October 15, 2012

HATIA--06


Na George Iron

Geti dogo lilifunguliwa kidogo, baada ya kuhakikisha aliyetegemewa kuingia ndiye alikuwa mlangoni lilifunguliwa zaidi.
“Mheshimiwa Mapulu!!!! Karibu nyumbani…..kama ndoto vile” sauti nzito ya kiume ilimlaki John aliyejibu kwa tabasamu hafifu.
“Matha yupo au na yeye alikamatwa??” John aliuliza wakati huo ilikuwa yapata saa kumi adhuhuri.
“Matha yupo lakini anakamuliwa na mshkaji mwingine” Alijibiwa kwa njia ya utani akaling’amua hilo akatoa kicheko kidogo.

“Dogo langu hili, linaitwa Michael Msombe muite Dabo M,ukishindwa kabisa muite Dabo” John alimtambulisha Michael kama mtu ambaye anamfahamu siku nyingi sana. Jina lake likageuka na kuwa Dabo.
“Mambo vipi bro!!!” alisalimia Michael MsombePoa Dabo naitwa Bruno…karibu sana”

“Asante sana” alijibu na geti likafungwa.

Haikuwa nyumba iliyotangaza umasikini hata kidogo lakini ilionyesha matumizi mabaya ya pesa kwa samani zisizokuwa na shughuli maalumu kulundikana pale ndani, usiku ule hakuona mtu yeyote zaidi ya Bruno akahisi huenda wamelala wengine lakini haikuwa hivyo hadi panapambazuka hali ilikuwa hivyohivyo.
Michael alishangaa lakini hakuuliza. Asubuhi yule John wa selo aliyekuwa akishindia kapensi kafupi kalikochakaa na wakati mwingine kumwacha uchi wakati akigombania vyakula walivyoletewa mahabusu wengine hakuwa yule tena alikuwa ameng’ara ndani ya nguo ya kulalia rangi nyeupe kabisa mkononi alikuwa na kikombe kikubwa kilichoongezwa uzito na maziwa yaliyokuwa ndani yake. John alikuwa tofauti sana hata rangi yake ilikuwa si ile iliyochafuka na kukosa maji ya kuoga walipokuwa selo.

“Michael kuna mtu yeyote aliyekuwa anafahamu uwepo wako ndani ya selo??.”

“Mh!!!! Hapana sidhani” alijibu baada ya kujaribu kufikiri

“Una uhakika kuwa hujawahi kuja kusalimiwa???”

“Hakuwahi kuja mtu yeyote pale kaka, we ulikuwa shahidi” aliendelea kusisitiza. John alitikisa kichwa ishara ya kukubali kisha akaifuata rimoti na kuitazama luninga kuubwa bapa iliyokuwa inamtazama kisha akaminya kitufe ikawaka, hakujishughuisha kuangalia ni chaneli ipi iliyokuwa inaupiga mziki wa zook, akajiondokea.
“Michael!!! Una uhakika na unalosema???” aliuliza tena macho yake mekundu yakiwa yanautazama mdomo wa Michael.
Swali hilo likamshtua Michael kwa nini lilikuwa likiulizwa sana, safari hii akachelewa kidogo kujibu

“Siku ile nilimpa namba za msichana mmoja yule afande sijui kama alipiga ama la lakini hakuwahi hata kuja pale mahabusu.” alijibu kwa sauti iliyokuwa na hofu

“Nipe namba ya huyo msichana na kuwa makini sana wakati mwingine unapojibu swali sawa!!!” alifoka kidogo John na Michael akakubali bila kuzungumza chochote. Baada ya kumtajia akaondoka, jambo la kushangaza ni kwamba John akuuliza mara mbilimbili na wala hakuandika hiyo namba mahali popote pale, ni kama alikuwa ameipuuzia hata Michael aliamini hivyo.
Siku hiyo ilipita huku Michael akipewa nguo za kubadilisha ambazo zilimkaa sawa kwenye mwili wake, japokuwa alikuwa na mawazo sana hakusita kukiri kwamba aliifurahia hali ya kuwa huru.

****

Majibu ya askari aliyekuwa na wasiwasi mkubwa machoni mwake yalimkera na kumshangaza sana Joyce Keto, alishindwa kuelewa kwamba ni kweli aliyezungumza naye kwenye simu alikuwa ni askari ama ni mtu alimletea utani. Kwa ghadhabu aliondoka kituoni pale.
Kwa nini nisimpigie simu huyo aliyejifanya askari!!! Alijiuliza Joyce huku akitembea kwa ghadhabu hakuwa na uhakika kama alikuwa akiyumba yumba ama la alichotambua ni kuwa alikuwa akisonga mbele. Moja kwa moja katika duka lililokuwa linauza vocha.

“Nisaidie Tigo ya mia tano!!” alisema Joy na mwenye duka akampatia baada ya kuwa ameisugua. Bila ya kujua ni mara ngapi alikuwa ameingiza ile vocha bila kuwa na umakini aishtushwa na ujumbe uliomtaarifu kuwa namba yake ilikuwa imefungiwa kutokana na kuingiza namba zisizokuwa sahihi, Joy alitamani kulia, aliitazama simu yake kwa jicho la hasira kama ni yenyewe ilikuwa imefanya makosa hayo ili kumkomesha. Kwa mwendo wa kukata tamaa akaanza kuondoka lakini akasita tena na kurejea dukani.

“Makao makuu ya tigo ni wapi, samahani lakini!!!”

“Bila samahani malkia!!....” alizungumza kwa lafudhi ya kichaga na kisha akamuelekeza Joy wapi ambapo kampuni hiyo ya simu imeweka makao yake.

“Asante sana….kwaheeri!!!” aliaga. Mwanzoni wazo lake lilikuwa kuondoka moja kwa moja na kuelekea hapo alipoelekezwa lakini njaa ilimkatisha kufanya hivyo, jicho lake liliangaza huku na huko kisha akajifikiria kwa muda pesa aliyokuwa nayo ilimruhusu kula wapi jibu likapatikana kuwa alitakiwa kula chakula cha bei poa sana ili mambo yaende sawia. Mama Fredi mgahawa jipatie chakula safi hapa.
Maandishi hayo yaliyoandikwa kwa mkaa yalimfanya Joyce atabasamu kisha akajiambia “Mahali sahihi pa Joyce kupata chakula chake kwa siku ya leo.” akanyata na kuingia kwa mtindo wa kuinama hadi akapata nafasi yake. Bila hata kutaja ni chakula gani alikuwa anahitaji alishangaa mbele yake ukiwekwa wali uliochanganywa na maharage, nyama moja, mchicha na kipande kidogo cha bilinganya, hakutaka kuhoji aliamini huo ndio utaratibu wa mgahawa wa mama huyo aliyekuwa muongeaji sana. Huenda hata ndio sababu ya kuvuta wateja wengi sana katika genge lake.
Baada ya kujiridhisha nafsi yake na chakula hicho kilichomgharimu shilingi elfu moja Joyce Keto alinawa mikono yake na kuondoka.

“Ngoja niandae mahali pa kulala kwanza maana dalili zote zinaonyesha kuwa nitalala Mwanza, na huu ugeni nisije nikapata tabu baadaye.” alijishauri na kukubali ushauri huo akaanza kuhangaika huku na huko hadi alipopata nyumba ya kulala wageni iliyomgharimu shilingi elfu kumi ikiwa na choo na bafu ndani.
Hakudumu sana katika chumba hicho baada ya kukizoea kwa dakika kadhaa wazo la kurejea tena Tigo lilimrudia, lakini kabla ya yote alijiweka maliwatoni na kuupasha mwili wake kwa maji baridi nguvu zikamrejea na uchangamfu ukachukua nafasi yake. Kosa dogo alilofanya Joyce liligeuka kuwa kubwa, ni baada ya kujiegesha kitandani na usingizi kumpitia. Alikuja kushtuka jioni ya saa kumi na moja.
Tayari huduma alizotaraji kuzipata tigo hazikuwezekana palikuwa pamefungwa tayari.
“Hee!! Saa kumi na moja.” alipayuka kwa nguvu akiwa pale kitandani lakini hakuwepo wa kumjibu hoja yake iliyokuja kwa mtindo wa kushtukiza. Alisimama kama anayetaka kuondoka ili awahi kitu lakini alirejea kivivu pale kitandani hakuwa na pa kwenda. Alijilaza pale alipotoka na kumkaribisha tena jinamizi wa usingizi lakini kabla hajachukua kiti na kuketi simu yake ya mkononi iliita. Ilikuwa namba mpya!! Mh!! Atakuwa mama yake Michael ama…sasa kwa nini atumie namba mpya…au!!!” alijiuliza bila kupata majibu, simu ikakatika!! Mara ikaanza kuita tena
“Hallo!! Mambo vipi dada Joy” upande wa pili ulianza kubwabwaja
“Poa nani mwenzangu samahani nilipoteza….”
Mimi Fredrick, haunifahamu lakini” ilimkatisha sauti ile baada ya kueelewa kuwa alitaka kujitetea kwa kudanganya.
“Wa wapi wewe??”
“Mwanza nimepewa namba yako na Michael yupo matatizoni, umeenda kumwangalia polisi???” iliuliza sauti ile kwa utulivu
“Nimeenda lakini sijamkuta….”
“Wamekwambiaje kwani??”
“Wamesema tu hayupo mi nikaondoka zangu”
“Dah!! Hata sisi wametwambia hivyo..wewe upo wapi sasa maana sisi wenyewe wageni hapa Mwanza”
“Mimi pia mgeni lakini nipo hapa Mitimirefu sehemu inaitwa Resting house, ukishuka tu hapa kituoni unapaona nadhani panafahamika” alijieleza Joy huku akiwa na furaha ya kupata wenzake katika vita moja.
“Haya kama tukiweza tutafika, kwa lolote lile tufahamishane sawa!”
“Msijali nitapenda sana mkija” alisisitiza Joy. Simu ikakatwa.
Baada ya saa zima akiwa anafanya tafakari mbili tatu alishtushwa na mlango wa chumba chake kugongwa kwa utaratibu maalum.
“Nani tena muda huu!!!” alijiuliza huku akiuendea mlango na kuufungua.
“Una vitu vingine zaidi ya huo mkoba mezani??” lilikuwa swali kutoka kwa sura hizi mbili ngeni kabisa machoni mwa Joy.
“Nyie ni akina nani??” aliuliza lakini hakujibiwa.
“Tuondoke haraka eneo hili” aliambiwa
“Twende wapi…nyie ni akina nani???”
“Ndugu zake Michael, chukua vyako tuondoke”. Joyce akatii amri na kukusanya vilivyo vyake na kuanza kuondoka hadi kwenye gari ndogo aina ya corolla safari ya kuelekea asipopajua ikaanza.
“Shem ujue nini yaani hii hali inashangaza sana mh!! Kumbe kweli anayekwenda jela si lazima awe na hatia…” baada ya kimya alikuwa ni John ambaye alikwa anajulikana kwa jina la Fredrick aliyeuvunja ukimya pale ndani. Mh!! Nimekuwa shem tayari!! Alijiuliza Joyce na kumalizia kwa tabasamu la kulazimisha bila kusema lolote.

Baada ya mwendo kidogo John alitoa pipi na kuwagawia wote waliokuwa pale ndani, ni Joyce pekee aliyekurupuka na kuibugia pipi ile, baada ya sekunde kadhaa usingizi mkali ulianza kuyafumba macho yake alijaribu kupambana bila mafanikio kuidhibiti hali ile, dhahiri alionekana kutambua janja hiyo iliyokuwa imechezwa dhidi yake lakini haukuwepo ujanja wowote ule Joyce akapitiwa na jinamizi la usingizi mkali sana.
Alikuwa amewekewa dawa za usingizi katika pipi!!!.
Alikuja kushtuka masaa manne baadaye na kujikuta katika chumba kikubwa cha haja ambacho kilikuwa na hewa safi sana yenye ubaridi bila shaka palikuwa na kiyoyozi.
Joyce alijinyoosha nyoosha huku akiyapikicha macho yake ili kujiweka sawa. Hapa ni wapi?? Alijiuliza, lakini kabla ya kupata jibu alisikia mlango ukifunguliwa kisha akaingia John ambaye alijitambulisha kwa Joy kama Fredrick.
“Mambo vipi Joy naitwa John….jisikie huru upo nyumbani” John alijitambulisha kwa Joy ambaye bado alikuwa anashangaa.
“Nimefikaje hapa….hapa ni wapi??” aliuliza Joyce, John ambaye alikuwa amevaa pensi pamoja na fulana kubwa iliouzidi mwili wake huku miguuni mwake akiwa na raba nyeupe.
“Hapa ndio nyumbani kwetu karibu sana” alisema John huku akiachia tabasamu hafifu.

*****

Michael Msombe alikuwa ametekwa na sinema aliyokuwa anaangalia katika luninga kubwa iliyokuwa sebuleni, hakupatwa na ukiwa wowote kwa kuondoka John na Bruno. Mdadi ulikuwa umemshika pale jambazi kuu lilipokuwa likipigwa na nyota wa filamu hiyo ambaye alikuwa ni Jackie Chan, Michael alikuwa ni kama amezama na kuwa mmoja wa wahusika wa filamu hiyo hadi pale aliposhtuliwa na kikohozi cha kujilazimisha kutoka katika upande wa mlango wa kuingilia.
Macho yake yalihama kutoka katika luninga na kuelekea pale mlangoni.
Alikuwa ni msichana ambaye hakuna mwanaume ambaye angesita kumuita mrembo, nguo fupi aliyokuwa amevaa iliyaruhusu mapaja yake meupe kuchungulia nje, wepesi wa kitambaa cha nguo hiyo ulionyesha mchoro wa chupi aliyokuwa amevaa ikiwa katika mfumo wa bikini, kinguo cha juu saizi ya mtoto wa miaka minne kilihalalisha nusu ya tumbo lake kuwa nje. Matiti yake kifuani yalikuwa na uwezo wa kukinyanyua kinguo hicho kwa umbali mdogo sana huku ule mchomo wa mbele ukionekana kumaanisha kamwe hajawahi kunyonyesha.
Sauti ya Michael ilipotea kabisa akajaribu kuilazimisha irejee ili aweze kumsalimia huyu kiumbe lakini iligoma kabisa.
“Mambo!!!!” alisalimiwa Michael kwa sauti laini sana iliyopenya katika masikio yake kisha katika koo na kuilainisha sauti yake hatimaye akajibu
“Safiii….karibu!!!” yule binti akaanza kusogea mahali alipokuwa ameketi Michael akimaanisha ameitikia wito, sehemu zake za nyuma zilikuwa zinatikisika kila hatua aliyopiga. Bila kutambua Michael akajikuta ameingia katika hisia nyingine na maungo yake kujikuta yakiinyanyua suruali yake, kwa haraka sana alichukua kitambaa kilichokuwa mezani na kujifunika lakini alikuwa amechelewa sana. Tabasamu zito kutoka kwa yule binti lilimpumbaza akabaki kama zoba.
“Naitwa Matha….unanifahamu sijui???...lakini haunifahamu”
“Yeah!! Sikufahamu nadhani”
“Ni mchumba wa John..unamjua??”
“Ndio John namjua!!!”
“Wewe unaitwa Michael eeh!!!”
“Umenijuaje kwani???” badala ya kujibu Michael aliuliza huku macho yake yakiendelea kumchunguza kwa chati binti huyu.

Matha Mwakipesile alikuwa amepewa jukumu kubwa la kumfundisha Michael jinsi ya kutumia silaha mbalimbali, John alikuwa ameamua kumchukua rasmi Michael katika shughuli zake za ujambazi.
Matha alimueleza Michael kwa utaratibu kabisa jukumu alilopewa, hali ya Michael iligeuka kuwa ya uoga sana hakuamini kuwa binti mrembo kama Matha anaweza hata kuwa na uwezo wa kushika bunduki sembuse kisu na kuua mtu. Mh!!! Usione ukadhani. Alisema kimya kimya Michael. Somo alilopewa na Matha halikuwa limemuingia hata kidogo, aliamini sasa alikuwa anapelekwa njia asiyoitaka hata kidogo. Kutoroka!!! Ndio wazo kuu lililomjia lakini atatoroka na kuelekea wapi. Akiwa bado katika mawazo hayo mara aliingia Bruno alikuwa mwingi wa furaha iliyojionyesha waziwazi, alimsabahi Michael kisha akaingia chumbani na kurejea tena baada ya muda mfupi akiwa amebadilisha nguo zake.
“Bruno nahitaji sana kwenda nyumbani, nimekaa hapa imetosha nadhani mama atakuwa akinitafuta sana.” Michael alimwambia Bruno baada ya kuwa amekaa kitako.
“John anakuja muda si mrefu utamweleza nadhani itakuwa vyema zaidi mi sijui lolote kuhusu wewe na John” alijibu kwa sauti iliyokuwa na uulizi ndani yake, Michael akatambua kuwa Bruno ameshtuka.
Baada ya masaa kadhaa John alifika na baada ya kuzungumza pembeni na Bruno alimfuata Michael.
“Nimeambiwa ombi lako si baya sana, lakini kabla sijakuruhusu naomba nikukumbushe kitu, unakabiliwa na kesi ya kumuua askari pale kituoni, una kesi kubwa ya kutoroka mahabusu hivyo umehalalisha kuwa ni wewe uliyemuua binti uliyekuwa naye nyumba ya kulala wageni, hizo ni kesi chache za halali zinazokukabili sijui kama zipo za ubakaji na wizi kwa kutumia silaha…kwa ufupi unarudi mtaani kupambana na hukumu ya kunyongwa baada ya fedheha ya kufanywa mke wa mtu gerezani….kama unaamini unaweza kupambana na haya yote peke yako mimi nitakusaidia nauli kesho uende mdogo wangu hata usijali.” alieleza John huku macho yake yakiwa yameutazama uso wa Michael aliyekuwa anaukwepesha uso wake kila anapogundua kuwa John anamwangalia.
Baada ya kumaliza kuzungumza hayo John aliyanyuka na kuondoka zake akimwacha Michael akiwa ameduwaa. Neno alilokuwa akilirudia mara kwa mara John kuhusu kuolewa na wanaume wenzake ni hilo lilimsumbua akili Michael hakuwa tayari hata kidogo kwa hiyo fedheha. Macho yalikuwa yamemtoka pima, aliingiwa na hofu ya kutoroka kwa mara ya kwanza!!.
“John!!! Kaka John.” aliita Michael kwa nguvu wakati John akikaribia kutokomea.
“Sema dogo!!!”
“Naomba basi walau niwasiliane na mama najua ananitafuta sana mh!!.”
“Polisi sio wajinga kama unavyodhani…wewe unamuwazia mtu ambaye kwa sasa anawasaidia upelelezi wa kujua wewe ulipo??? Wewe kumuona mama yako haina tofauti na kuonana na polisi” alijibu John Mapulu kisha akacheka. Neno hilo nalo likamshtua Michael na kuamini kuwa lilikuwa na ukweli ndani yake na mama yake huenda anaweza kumsaliti.
“Kwa hiyo hata Joyce Keto anaweza kuwa anasaidiana na polisi?.” alijikuta akiuliza.
“Tena kwa ukaribu sana…nakutakia safari njema Michael” alifungua mlango na kuingia ndani.
Kesho yake hakuondoka!!!!!
Pabaya hapo!!

No comments:

Post a Comment

Recent Posts