Friday, September 21, 2012

HATIA--05


Na George Iron

MUGUMU SERENGETI

Usumbufu aliokuwa akiupata kutoka kwa mama yake Michael kuhusu mwanaye ulimkosesha amani Joyce Keto sasa alikuwa ameeamua kubadili laini ya simu yake ili aweze kuwa na amani walau kiduchu. Mara moja moja alikuwa akiiweka ile laini na kusoma baadhi ya jumbe zilizokuwa zimeingia kisha kuitoa katika simu.
“Mwenye namba 0657727324 amekupigia simu saa……” ulisomeka ujumbe katika simu yake.
“Mh!! Atakuwa nani huyu jamani…” alijiuliza Joyce akiwa katika kitanda chake katika nyumba aliyopanga kwa muda. Haraka haraka alizinakiri zile tarakimu katika karatasi na kisha akatumia simu yake nyingine kupiga.
“Hallow!!” upande wa pili ulipokea ilikuwa sauti nzito ya kiume.
“Samahani kaka, nimekuta ujumbe wako kwamba ulinipigia simu lakini sikuwa napatikana” alijieleza Joyce
“Hii simu wanatumia watu wengi, afande Matiko Mwanza hapa je kuna uhusiano wowote” aliuliza
“Ahh!!! Sijaelewa.”
“Labda kuna ndugu yako ni mahabusu maana hawa ndio wanapiga piga simu sana kwa ndugu zao, kwani hiyo namba yako ni ipi” aliuliza na Joy akamtajia naye akawa anaiandika.
“Aaaah!! Kuna ndugu yako huku tena ana siku nyingi sana anaitwa Michael Msombe” alijieleza yule afande.
“Nani Michael????......upo wapi afande wewe, kwani amefanya nini tena…aah!!! Umesema Mwanza” alijikanyaga kanyaga Joyce baada ya kupokea taarifa hiyo.
“Mwanza kituo kikuu cha polisi…usiku mwema” aliaga na kukata simu.
Bila kuchukua ruhusa kazini, siku iliyofuata Joyce alidamka mapema sana na kupanda mabasi yaendayo Mwanza, ni mwendo wa masaa manne hadi matano kulifikia jiji la Mwanza. Siku hii aliiweka hewani ile namba yake ya siku zote na tayari alikuwa amempigia mama yake Michael na kumweleza kuwa Michael yupo Mwanza na anakwenda kuonana naye.
“Mwambie anipigie kuna tatizo huku sawa mwanangu, asante eeh!!” alijibu mama yake Michael kwa furaha.
Safari ilikuwa ndefu sana lakini hatimaye wakalifikia jiji la Mwanza hii ni baada ya kupanda mabasi mawili kwani basi la moja kwa moja halikuwepo siku hiyo.
“Naitwa Joyce Keto….natokea….”
“Sema shida yako…” alikatishwa na polisi aliyekuwa kaunta
“Kuna ndugu yangu hapa anaitwa Michael Msombe nimekuja kumwona nasikia amekamatwa”
“Anaitwa nani na amekamatwa lini???” aliuliza kwa hofu afande
“Sifahamu….”
“Haya subiri hapa dakika mbili…. Una uhakika wewe ni ndugu yake” alihoji Joy akatikisa kichwa kuashiria kukubali
“Hakuna mtu kama huyo hapa” lilikuwa jibu la afande.
“Hapa ndio central….” Aliuliza Joyce
“Ndio hapa kwani hujui kusoma” alijibiwa kwa mkato na yule afande ambaye alionyesha kuwa hakupenda kuzungumza na Joyce.

****

Taratibu Michael na John Mapulu wakawa marafiki ndani ya lock up, mara kwa mara walipiga stori za hapa na pale kuhusiana na maisha halisi huku simulizi za John zikimsisimua sana Michael ambaye hakuwa na jambo lolote lile la kutisha nje ya chuma hizo za mahabusu.
“Mimi ni mbaya naua dakika yoyote ile kisha nasahau!!!!” alisisitiza John na kumwacha Michael mdomo wazi akiwa haamini kama yupo karibu na mtu wa hatari kiasi kile, japokuwa John hakuwa na mwili uliojaa sana lakini alikuwa na makovu mengi sana kuonyesha kwamba amebobea.
“John Mapulu!!!!!” iliita sauti ya afande aliyekuwa ameikaza sura yake kana kwamba analinda mahabusu hata mmoja asitoroke, huku John akiamini sauti hiyo ilikuwa ni ishara kwamba mahabusu mpya ameingia hivyo aje kumpokea la! Haikuwa hivyo John baada ya siku nyingi alihitajika nje ya selo hiyo, labda kwa ajili ya mahojiano!!!, labda kupelekwa mahakamani, au kuachiwa huru kabisa!!! Hapana haiwezekani kwa muharifu kama huyu.
“Dogo kama nisiporudi mamlaka yote sasa juu yako, naweza kuwa napelekwa sehemu inaitwa ‘Sitaki maelezo’ huko ni hatari sana mdogo wangu hakuna mwanaume hata mmoja anayeweza kusita kutoa machozi, wanatesa vibaya sana na bila kujali lolote unaweza ukafa na usishtue jamii, na ujasiri wangu wote kule napaogopa sana, ukifanikiwa kutoka salama wewe si mwanaume tena!! Kule wananyanyaswa wenye makosa na wasio na makosa, hakuna huruma kule” kwa mara ya kwanza Michael akaisoma hofu aliyokuwa nayo John baada ya kuhitajika nje ya selo hiyo.
Michael hakuwa na la kuongezea, moyo wake ulidunda mara mbili ya mwendo wa kawaida huko Sitaki maelezo aliwahi kupasikia tu kuwa ni kituo cha polisi cha Mkuyuni lakini maalumu kwa ajili ya mahojiano na watuhumiwa wa makosa ya jinai. Mh!! Hivi na mimi nina kosa la jinai eeh!!! Alijiuliza Michael na kuzidi kupatwa hofu.
“John!!! Nakusubiri wewe!!!” alizidi kusisitiza afande, kwa unyonge John akaiangalia selo na kutoka nje, suruali aliyoivaa haikuwa na uwezo wa kukaa kiunoni. Alikuwa amekonda sana!!
Michael alibaki mkiwa japo hakuna aliyethubutu kumsumbua kwa lolote amani haikuwepo nafsini mwake, huku akiwa anaamini fika kuwa John Mapulu hatarejea, muda wa saa tatu usiku akiwa amelaa baada ya kuwa wamehesabiwa alimsikia John akirudishwa pale mahabusu.
“Kwa kesi niliyonayo sasa hivi wataninyonga!!! Sipo tayari kufa kwa sasa” ni maneno ya kwanza kabisa John kumnong’oneza Michael ambaye alikaa kitako kumsikiliza vyema.
“Kwanini kaka unasema hivyo na imekuwaje umerudishwa hapa ndani??” alihoji Michael kwa mtindo uleule wa kunong’oneza.
“Nitakueleza lakini kwa sasa hebu ngoja….watu wote wamelala hapa ndani??.”
“Nahisi watakuwa wamelala ni muda mrefu sana tangu waache kuzungumza” alipojibiwa hivyo aliingiza mkono wake mmoja sehemu zake za siri na kuibuka na kitu ambacho Michael hakukifahamu si tu kutokana na giza hapana hakuwahi kukiona kabla.
“Dogo umewahi hata siku moja kufikiria kuwa maisha yako yanaweza kuishia gerezani??.”
“Hapana kwani vipi??.”

“Vipi kuhusu kufanywa nyumba na mwanamme mwenzako??.”
“Nyumba?? Ndio nini!!!” aliuliza kwa mshangao lakini kwa sauti ile ile ya chini
“Kuolewa!!!”
“Hapana na haitatokea…”
“Ukienda jela utaolewa bila kupenda na mwishowe utazoea.” alijibu John huku akijikuna mgongo wake, Michael alibaki anashangaa kama aliyeambiwa mke wake ana mimba isiyokuwa yake.
“Una maana gani??.”
“Namaanisha utaolewa kama unapenda kwenda jela.”
“Sipendi kwenda jela!!!.” bila kutarajia alijikuta anamjibu
“Mimi pia sipendi kunyongwa hadi kufa ni heri nife kwa risasi…..hivi unafahamu kesi yako hukumu yake ni ipi??.”
“Hapana sifahamu!!.”
“Unapenda kifo cha aina gani??.” John alimuuliza
“Mhh!! Sipendi kufa.”
“Basi wao watakunyonga hadi ufe maana wewe uliua!! Utajisikiaje siku unahukumiwa??” aliuliza kama swali la kawaida kabisa
“Lakini mimi sikunyonga!!!” alijitetea Michael bila kujua kwamba pale hapakuwa mahakamani, John Mapulu akacheka kwa sauti ya juu kidogo.
“Mimi leo hii usiku natoroka sijui wewe mwenzangu” John aliyatamka hayo kama vile anayeaga kwenda msalani mara moja na kurejea tena baada ya muda mfupi tu.
“Unatoroka!!! Kiaje mimi a a siwezi.” aligutuka Michael
“Haya mimi nilikuwa nakuaga tu!! Kama vipi utamsalimia bwana mmoja anaitwa Dunga Dunga kama ukipelekwa gereza la Butimba na yeye anasubiri kunyongwa kwa hiyo utakuwa naye, yeye ni bingwa wa kuoa wenzake halafu yeye kuolewa hataki lazima atakuchangamkia, lakini kama akiwa amenyongwa tayari sina budi kusema alale pema peponi.” alimaliza kwa kucheka hasahasa baada ya kukumbuka kuwa amesema alazwe pema peponi. Muharifu kama huyu!!!
“…….halafu kama wasipokunyongea hapa Mwanza basi wanaweza kukurudisha kwenu……huko Dar gereza moja hivi linaitwa Keko. ni heri ufanye sala kwa Mungu wako unayemwamini wakunyongee hapahapa Mwanza….” Aliongezea John.
Mh!! Nifanye sala kwa ajili ya kuchagua mahali pa kunyongewa??!!! Alishangaa Michael.
Michael alishikwa na hofu kuu ni kama John alikuwa ameshika kitanzi kwa ajili ya kumnyonga baada ya hukumu kupitishwa. Fundo la hasira lilimkaba kooni, alitamani sana kila mtu afahamu kuwa yeye hana makosa lakini hilo halikutokea.
“Mapulu nimesema sipo tayari kufa….”
“Umewahi kusikia mtu ananyongwa halafu anapona??.”
“Hapana!!!”
“Sasa wewe unasemaje hutaki kufa wakati upo tayari kunyongwa???” aliuliza kwa sauti iliyodhihirisha kukerwa na msimamo wa Michael.
“Tuondoke wote John.”
“Sio tuondoke sema tutoroke!!!.” John alimrekebisha Michael usemi wake. Michael akalazimisha kutabasamu. Wakalala!!
Ni kama vile John alikuwa na saa ameitegesha, usiku wa manane kila mahali pakiwa kimya alisimama wima kwa tahadhari kubwa akawaruka wenzake kwa kunyata hadi akaufikia mlango wa stoo iliyokuwa inatumika zamani sana, kufuli lake lilikuwa kubwa lakini lenye muundo wa kizamani. Akachomeka kifaa alichomuonesha Michael baada ya kuingia, kwa muda wa sekunde kama tatu kufuli likasalimu amri.
Mlango ulikuwa mgumu sana kufungua na ulielekea kumshinda John.nimuamshe Michael!!! Hapana. Alijiuliza kwa sekunde kadhaa kisha akaingia chumba kimoja akawaamsha watu wawili hawa walikuwa na kesi ya kukutwa na bunduki. Hakika John alikuwa hajakosea baada ya sekunde kadhaa mlango ulikuwa wazi.
“John Mapulu!!!!!” ilisikika sauti kali ikitokea mlango mkuu wa kuingizia mahabusu, John na wenzake wawili walibaki wakishangaana kwani tayari walikuwa wamefungua mlango. Jonh aliwaonyesha ishara ya kukaa kimya nao wakatii.
“John!!! mteja wako mpya huyu hapa….ingia huko nenda moja kwa moja huko mwisho” ilisikika sauti ya afande akitoa maelezo kwa mahabusu. Haraka haraka John alivyosikia mlango umefungwa aliwaacha wenzake wawili waliokuwa katika azma moja na kumuwahi huyo mahabusu mgeni asijue nini kinaendelea.
“Lala hapo hapo wasikuzingue hao!!!” John alimkaribisha yule mahabusu mahali pazuri kabisa naye akashukuru na kujilaza.
“Michael…..Mi…. amka wewe” John alimtikisa Michael na yeye akiwa na kumbukumbu sahihi kabisa alisimama wima na kumfuata John Mapulu.kuolewa!!kuteswa ….kunyongwa…hapana bora kutoroka!! Ni uamuzi alioufikia Michael akauvaa ujasiri.
“Nikikamatwa nimekwisha!!!!” alijisemea Michael bila kumpa nafasi John kugundua kwamba alikuwa na wasiwasi mkubwa. Mlango ulikuwa wazi Michael akatangulizwa kisha wale wengine wawili ambao John alitokea kuwakubali ghafla kisha akajitosa ndani mwenyewe ukawa umebaki mlango mmoja pekee waweze kufika nje na kuwa huru.
Kiongozi wa msafara akiwa ni John hivyo alisikilizwa kwa kila kitu. Wakati huu aliwasihi wenzake watulie tuli tena wakatii. Alifanya kitendo cha dakika chache kuvua suruali yake, kuchuchumaa chini kisha akapeleka mkono wake katika sehemu ya haja kubwa akaibuka na simu ndogo nokia 1100 ile ya tochi.
Michael akakodoa macho lakini wale wengine hawakushangaa kwani huo mtindo walikuwa wanaufahamu mtindo huo unaitwa kupandisha na kushusha. John akamsoma Michael usoni alivyoshtuka akajenga tabasamu bandia bila kusema neno lolote. Simu iliwashwa, ujumbe ukatumwa kisha ikazimwa baada ya kujibiwa ujumbe.
“Dakika tatu zinazokuja tutakuwa nje, msiwe na papara zozote zile ili tufike salama!!!” alizungumza kwa kumaanisha John Mapulu, Michael alikuwa anatetemeka, alitambua kuwa hakuwa na hatia lakini sasa alikuwa anajiingiza katika hatia ya ukweli. Lakini kipi bora kunyongwa bila hatia au ukiwa na hatia!!! Alijiuliza lakini alikuwa amechelewa sana kupata jibu litakalompa maamuzi sahihi mlango wa pili ukawa wazi.
“JOHN Mapulu….kuja hapa…kuja hapa haraka” ilisikika sauti ya amri ni sauti John aliyoifahamu ilikuwa sauti ya mpelelezi wa kesi yake Sajenti Romagi, mpelelezi aliyesifika kwa ukatiri wake

Mkojo wa moto kabisa ulikuwa umeshapenya katika suruali ya Michael, alikuwa muoga kuliko wenzake hii ni kwa kuwa hakuwahi kuzoea hizo pilika pilika. John alisimama thabiti akakuna kichwa chake kutafuta maamuzi sahihi ama kurejea na kuitikia wito ama kuendelea na safari yao ya hatari kabisa.
“Twendeni!!!” aliamuru John, akafuatiwa nyuma na kundi la watu watatu wote wanaume lakini mmoja akiwa anatetemeka sana kama mwanamke huyo alikuwa ni Michael. mlango wa kutokea nje ulikuwa umefunguliwa na vijana ambao walikuwa wameziba nyuso zao kwa kutumia vitu kama soksi kubwa hivyo sura zao hazikuonekana. Hawakuzungumza kitu lakini John alielewa kipi kinachoendelea, upepo wa nje majira ya usiku ulipokelewa vilivyo na mapafu ya Michael na kumsahaulisha kosa kubwa alilokuwa amelitenda kosa la kutoroka!!!! Akiwa hajui la kufanya na wapi pa kwenda John Mapulu alimshika mkono wakaanza kutokomea taratibu kuelekea walipojua wao lakini Michael alikuwa kama kipofu anayefuata mkondo.
Hatua kadhaa mbele Michael akiwa ameamini tayari wapo huru bila kupata usumbufu wowote katika giza walimkuta askari aliyekuwa lindoni akiwa amejiegemeza ukutani, John akamshtukia kuwa tayari alikuwa ameuchapa usingizi maeneo yale ilisikika harufu kali ya bangi bila shaka kabla ya kusinzia askari yule alivuta misokoto kadhaa ya mmea huu halali katika nchi ya Jamaika.
Michael ambaye muda wote alikuwa anatetemeka alimshuhudia John akinyata kwa tahadhari kubwa na kumrukia yule askari kilichofuata ni kitendo cha John Mapulu kuwa juu ya askari huku mikono yake ikiwa imelikamata koromeo la huyu kiumbe barabara, baada ya dakika kadhaa akamwacha huru, licha ya kuachiwa huru hakuweza hata kusema neno. Alikuwa maiti!!!
“Washenzi sana hawa!!!” alisema John kisha akampa ishara Michael amfuate, wale waliofungua mlango na akina John wakatoka walikuwa wamepita njia nyingine pamoja na wale wawili wenye kesi ya bunduki waliopata upenyo wa kutoroka pamoja na John baada ya kuamshwa wasaidie kufungua mlango. John tayari alikuwa na bunduki mkononi nani wa kumtisha kiumbe huyu hatari linapokuja suala la kutumia bunduki!!!! Michael alijiona muuaji na anayezidi kupotea njia pumzi za uhuru alizozikurupukia sasa zilikuwa zinamuwasha zaidi ya kawaida. Hatua kwa hatua, mtaa kwa mtaa, hatimaye walikuwa katikati ya kundi la raia wema ndani ya daladala zinazoelekea Nyakato Mecco nje kidogo ya jiji la Mwanza.
Michael bado alikuwa kipofu!!!

No comments:

Post a Comment

Recent Posts