Thursday, November 8, 2012

HATIA----12


MTUNZI: George Iron Mosenya

CONT: 0655 727325

SEHEMU YA KUMI NA MBILI

"Kwa hiyo Joyce ametoroka ama ame.."

"Hapana hajatoroka wala hajafa.....tatizo ni kwamba baada ya miezi minne atajifungua" alijikakamua na kujibu Mzee Bushir.

"Joyce ni mjamzito!!!!!"

"Ana mimba" alijibu Bushir, John akalegea akakaa chini, hakupenda kabisa kuisikia taarifa hiyo. Hiyo ndio zawadi alikuwa ameiandaa kwa ajili ya kumpelekea Michael kwa ukarimu wake na kumrejesha Matha katika himaya yake, zawadi ya pikipiki pekee ilikuwa haijatosheleza. John akajikuta katika dimbwi kubwa la mawazo, moyo wake ulijutia kitendo cha kumficha Joyce kwa muda wote huo. Michael hatanielewa kabisa!!!! alisema John, Bushir hakuelewa lolote hakuwa akimjua Michael.

Hakuwa na jinsi aliamua kuendelea na zoezi la kusafisha bunduki huku wote wakiwa kimya sana, kitendo cha Joyce kuwa mjamzito kilimtia uchungu sana na kuikaribisha shubiri ya hatia kuanza kumshambulia, hakuwa akimuogopa Michael hata kidogo lakini pia hakutaka kuweka udikteta mbele ati kisa yeye ni mbabe mbele ya Michael.



*****



Tumbo lake lilikuwa halijachomoza bado, kipande cha limao kilikuwa pembeni ya kitanda chake. Alikuwa amejilaza huku akilitazama panga boi lililokuwa linapambana na joto lililokuwa linataka kuingia humo ndani, bila shaka katika mpambano huo panga boi lilishindwa ndio maana akatumia leso aliyokuwanayo kujifuta jasho lililopenya katika vinyweleo vyake. Mawazo yake makuu yalikuwa juu ya kiumbe aliyekuwa amejihifadhi katika tumbo lake, wazo la pili lilikuwa juu ya utata uliopo katika kiumbe huyo asiyekuwa na hatia kwa upande wake lakini mama yake alifikiria kwamba kiumbe huyo naye pia ana hatia kwanini aingie sehemu isiyokuwa salama.

Mwanamama huyu mtarajiwa alisita kumuwazia kiumbe aliyebebwa na tumbo lake baada ya kusikia hodi mlangoni. Aliuvuta mdomo wake na kumlaani huyo aliyekuwa anaugonga mlango wake, hakutaka usumbufu wowote ule siku hiyo alikuwa ameamua kupumzika na kujichukulia maamuzi ya kipekee.

"Ulikuwa umelala nini??" aliulizwa bila hata kusalimiwa

"Wala kwani vipi??"

"Niazime elfu mbili, baba Rozi akija nitakurudishia" ilikuwa sauti ya upole kabisa ya mama Rozi sauti ile ilielezea waziwazi shida. Matha Mwakipesile hakujibu kitu aliingia ndani na kurejea na noti ya shilingi elfu mbili akamkabidhi mama Rozi, akashukuru na kuaga. Wakati anataka kurejea ndani alimuona mtu kwa mbali chini kabisa, alidhani mwanzoni kuwa amemfananisha lakini hakuwa amemfananisha.

Mbiombio akashuka akiwa na kanga moja hakujalisha ni wangapi watamuangalia japo alijijua kabisa ni kiasi gani ana makalio makubwa na mitikisiko yake ni kanga hiyo pekee ingeweza kuijibu kuwa ni kiasi gani inaipa shida. Mwendo wa harakaharaka akaona kama haumsaidii akaamua kukimbia kumuwahi mtu yule, vijana wavuta bangi na wasiokuwa na kazi walianza kupiga miluzi, Matha hakujali lolote. Alishawazoea!!!

Alilipita hilo kundi kama vile upepo na kuendelea mbele, akiwa hajategemea tukio kama hilo kumtokea Matha alihisi kuguswa na mkono wa mtu, kuna bwana alikuwa amemshika Matha makalio. Miluzi ikazidi kwa sababu ya tukio hilo, hasira ikamkumba Matha. Yule mwanaume akaleweshwa sifa na ile miluzi akaanza kukimbia kumfuata Matha ili amshike tena na kujizolea sifa zisizokuwa na tija.


Macho makali na maangavu yakamtoka Matha akahisi kudhalilishwa na mtu dhaifu sana, akauvua urembo wake akauvaa umafia aliofunzwa na John Mapulu, Matha akauvaa ukichaa wake akaudaka ule mkono kwa kutumia mkono wake wa kushoto. Mkono wa kuume ukatamani nao kufanya walau kazi kidogo, Matha akauruhusu, ngumi moja imara ilitosha kuuchana chana mdomo wa mtumiaji huyu wa madawa ya kulevya ambaye shibe kwake ni hadimu sana, damu ilibakia katika mkono wa Matha wala haikumshtua alishayazoea matukio hayo. Mzuka wa mapambano tayari ulikuwa umempanda. Akamuona yule kiumbe alifaa sana kwa kushushia mzuka huo. Mwanamke huyu jasiri alifanya kitendocha ghafla lakini cha maajabu. Alijitupa hewani kwa mzunguko wa teke la Vandame, teke la kwanza likamkosa lakini like la pili likatua sawia shingoni. Akatua chini kama mzigo. Tendo alilolifanya Matha mwanamke wa kawaida hawezi kulifanya lakini MATHA si mwanamke wa kawaida!!!

Alipomaliza kumuadabisha kelele hazikuwa kwake tena bali alikuwa akizomewa yule aliyeadhibiwa, Matha alikuwa amempoteza machoni mtu aliyekuwa anamfuatilia lakini alijipa moyo kuwa atakuwa ameingia stendi.

Akaamua kuingia hapo ndani, kwa macho makali kabisa ya kijambazi aliangaza haraka haraka ndani ya dakika tatu tayari alikuwa amemtia machoni.

"Michael!!!!" aliita Matha, bado alikuwa na ari ya kijambazi. Michael aligeuka na kukutanisha macho yake na Matha, alitaka kukimbia pasipo sababu Matha akaligundua hilo akamdaka mkono, Michael hakutegemea Matha huyu ambaye huwa anamsukuma anavyotaka wakiwa kitandani anaweza kuwa imara kiasi hiki, hakuweza kuutoa mkono wake katika mkono mmoja wa Matha.

"Unaenda wapi Michael"

Michael hakujibu, Matha akamkokota hadi pembeni kidogo ambapo waliweza kusikiana wao wawili tu. Matha akamtazama Michael machoni kisha akamwachia

"Naomba unipe dakika mbili tu nizungumze ukimaliza endelea na safari yako, safari ya kumkimbia mwanao, safari kafiri ya kuyakimbia majukumu!!! Michael samahani kama nakulazimisha, kuwa huru wewe ondoka lakini kamwe sitakiua kiumbe ndani ya tumbo langu, nipo radhi John aniue lakini si mimi kuua, nilitegemea muunganiko huu wa damu ndio ungetupa akili ya kutanua penzi letu lakini kwako haikuwa hivyo, ni wapi sasa waelekea??? sitaki kujua jibu la swali lako, kwani najua ni wapi unaelekea, unatokea katika uanaume wako kamili na kuukimbilia ushoga kwa ufahari mkubwa.

Nenda Michael, nadhani umenichoka na unatamani kuolewa gerezani, nenda Michael nenda!!!" alishindwa kuendelea kuzungumza Matha donge la hasira lililokuwa limemkaba kooni likapasuka na kuleta sayansi ya ajabu kuliko zote duniani, uchungu wa moyoni unaosikika kooni na kifuani kisha kutokea machoni kama machozi na kujihifadhi tena mwilini kama majonzi makubwa. Kwa haraka haraka akaanza kuondoka, mkono wake ukawa unamsaidia kuyafuta machozi kwa nguvu zote, machozi yakakaribisha kamasi nyepesi hasira kali ikamfumba macho Matha barabara mbovu ikamkaribisha kipofu huyu wa muda akajikwaa na kuisalimia ardhi kwa heshima zote, kichwa, kidevu, mikono, miguu na tumbo vyote vikaibusu barabara!!!! Matha hakupata hata nafasi ya kupiga kelele akatulia tuli.

Michael akaliona tukio lile, begi lake dogo likamponyoka lakini hakujua kama limeanguka akaanza kutimua mbio, Matha alikuwa ametulia tuli


*******


Joyce Keto alikuwa amejikita katika kucheza game katika kompyuta ndogo iliyokuwa chumbani kwake, tayari alikuwa ameyazoea maisha ya kufugwa, miezi kadhaa aliyokuwa amekaa hapo bila kuwasiliana na upande wa pili wa dunia ulikuwa umetosha kumbadilisha, alipata kila alichokitaka katika nyumba ile aliishi na familia ile kama yupo nyumbani kwao, japo alipata tabu sana siku za mwanzo kuzoea lakini baada ya kipindi hicho kirefu alizoea.

"Da Joy baba anakuita!!!" aliitwa na mtoto wa bwana Bushir aliyeitwa Davda alikuwa na asili ya kihindi.

Joyce Keto hakujibu kitu aliendelea kucheza game kisha baada ya dakika kadhaa aliinuka na kuelekea katika wito.

"We!! Davda yupo wapi mheshimiwa" aliuliza Joyce. Davda akamweleza akatoweka kuelekea katika wito.

"Neh neh papa!!!" Joyce alizungumza akimwambia Bushir, Bushir akajilazimisha kucheka. John akajua kuwa Bushir alikuwa na utani na Joyce.

"Shkamoo bosi!!!" alimsalimia mgeni aliyekuwa na Bushir. John Mapulu naye hakujibu bali alicheka japo si kicheko halisi, Joyce akachukua nafasi katika kiti kilichokuwa wazi, akaiunganisha miguu yake katika staili ya kukunja nne, kinguo kifupi alichokuwa amevaa kikayaweka mapaja yake wazi, kwa Bushir lilikuwa jambo la kawaida lakini kwa John moyo ulighafirika akahisi anaingizwa majaribuni.

"Mambo vipi Joy....unanikumbuka???"

"Hapana tangu nizaliwe ndo nakuona mara ya kwanza hata ndotoni sijawahi kukutana nawe" alijibu Joy, John akacheka. Hakika Joy asingeweza kumkumbuka John kwani kwa sasa alikuwa ana afya tele tofauti na awali alipokuwa ametoroka rumande.

"Naomba niwaache kidogo!!" aliaga Bushir

"Naitwa John.......John Mapulu" alijitambulisha

"Mara ya mwisho nilikuona ukiwa unamtesa bwana mmoja kule Mwanza ni nani yule??" aliuliza Joyce huku akilamba kipande cha limao. John hakuwa na la kujibu.

"Mimi!!!!!"

"Ndio wewe John, japo umebadilika, nilikuwa nimekusahau lakini sio jina lako kamwe sijalisahau"

John alijaribu kupambana na wasiwasi uliomkumba kwa kupiga funda kubwa la juisi iliyokuwa mezani, akafanikiwa.

"Utajua siku nyingine" akajibu kwa amri, Joyce Keto akanywea.

"Unamfahamu aliyenibaka" aliuliza Joyce

John akashindwa tena kujibu, Bushir alikuwa amesahau kumwambia John kuwa tukio la kubakwa alilofanyiwa Joyce liliathiri akili yake na kumfanya kuonekana kama kiumbe wa ajabu asiyeogopa kitu.

"Nitampata!!!!" alijibu John swali ambalo hakuwa ameulizwa

"Ukimpata utanipa na mimi nimtese kama mlivyomfanya yule wa Mwanza" alizungumza Joyce akikumbuka tukio la kumuona John akimuadabisha mateka wake jijini Mwanza.

"Usijali!!!!"

“Yule mjomba wetu mzima…”

“Mjomba? Yupi?”

“Yule ambaye mlikuja naye siku zile kunichukua ….” Joyce alikuwa akimaanisha Bruno. John akaishia kucheka bila kujibu. Joyce naye akafanya tabasamu!!!

Hawakuzungumza zaidi!!


*****


Hofu aliyokuwa ameipata Michael ingeweza kumletea uwendawazimu kichwani kama tu asingekuwa jasiri wa kukubaliana na hali, jambo zuri ni kwamba walikuwa jirani sana na kituo kikubwa cha mabasi hivyo usafiri wa kukodi halikuwa jambo lenye usumbufu sana.

Ndani ya dakika mbili Michael alikuwa amepata wasaidizi wa kutosha wengine walikuwa kazi yao ni kulia wengine walimgusagusa Matha Mwakipesile kama vile walikuwa wanampima homa kwa njia ya hisia za mkono. Matha hakutikisika, baada ya ushirikiano mkubwa Matha alikuwa ndani ya 'Taksi' safari ya kuelekea hospitali ya mkoa ya Bugando!!! Hakuwa akijitambua kwa lolote, fahamu zilikuwa zimeuacha mwili kwa muda.

Wazo la Michael kutoroka likawa limeishia pale.



******


Umati wa watu katika jumba la kifahari alilokuwa anaishi John na Bruno kabla ya ujio wa Michael ulimshangaza kila mtu, ulikuwa ni msiba wa aina yake, watu wote walikuwa wamevaa sare sare, wanaume walikuwa wamevaa suti nyeusi huku akina mama wakiwa na mavazi yao ya vitambaa vyeupe, kila mmoja alipendeza. Katika kundi la wanawake wale ni mwanamke mmoja tu aliyemshtua Michael, huyu kwa kila kitu alifanana na Joyce Keto, msichana ambaye kwa namna kubwa sana alikuwa amechangia yeye kuwa katika janga hili lililotawaliwa na Hatia.

"Ametoka wapi??? au nimemfananisha" alijiuliza Michael wakati huo akijipenyeza katika kundi la wanaume na kuingia katika kundi la akina mama, lengo likiwa kuhakikisha kuwa aidha yule ni Joyce ama la!!.

"Mambo vipi dada!!" alimsalimia, yule mwanamke aligeuka na kuanza kumshangaa, wakati wakiwa bado wanashangaana Michael alihisi kuguswa begani, mwanzo alipuuzia hadi pale Joyce alipomwambia kuwa anaitwa. Alipogeuka alikutana na sura ya Matha ikiwa inatabasamu kinafiki.

"Mamaaaaaaaaaaaaaaaa!!!!!!" alilipuka kwa kelele kubwa Michael.

"Vipi kaka nini???" Michael aliulizwa na mtu aliyekuwa pembeni yake.

"Ah!! ni ndoto kaka dah!!!" Michael alijibu huku akiyapikichapikicha macho yake ili aweze kuipata nuru mbele yake, nuru iliyokuwa imemezwa na usingizi, usingizi ulioambatana na ndoto, ndoto ya ajabu, ndoto ya kifo cha Matha na marejeo ya Joyce Keto. Ah!! ni ndoto tu Matha hawezi kufa!! aliwaza Michael na kupuuzia alichokiota. Pia alijenga tabasamu baada ya kuyakumbuka maneno ya mama yake aliwahi kumwambia ukimwota mtu amekufa, huyo hafi.

"Lakini Joyce hivi atakuwa wapi yule binti!!!" alijiuliza, hakuwepo wa kujibu. Majira ya saa kumi na moja jioni majibu kutoka chumba cha uangalizi alichokuwa Matha yalitolewa. Hakuwepo mtu mwingine wa kuyapokea zaidi ya Michael ambaye ndiye alimleta.

Majibu hayakuwa ya kufurahisha sana, kwani maombi ya Michael yalikuwa juu ya mimba alitamani sana itoke lakini wala jambo hilo hakulisikia kutoka kwa daktari.

"Jitahidi sana, hakikisha anapata pumziko la kutosha na matunda ale mara kwa mara."

"Hamna shaka dokta" alikubali Michael. Saa moja usiku Michael aliruhusiwa kumchukua mgonjwa wake, pesa ya ziada aliyobaki nayo mfukoni alilipia matibabu na usafiri wa kurudi nyumbani, safari nzima walikuwa kimya hadi wakafika nyumbani kwa Matha, Michael akamsaidia Matha kupanda ngazi taratibu hadi wakafika chumbani. Siku mbili mfululizo Michael alikuwa anashindia nyumbani kwa Matha akimuuguza, Bruno hakuwa akifahamu ni wapi huwa anaenda na wala hakujali sana kwani ni mtoto wa kiume. Furaha ya Matha ilirejea tena kutokana na upendo wa Michael.

Maisha yakaendelea!!!

Haikuwa kawaida ya Michael kulala nyumbani kwa Matha, nafsi haikumvusha hadi kuufikia ujasiri huo. Lakini siku hii ya ijumaa tulivu kabisa Michael alijikuta akifanya mambo kinyume na matakwa yake.


Ilianzia kwenye sherehe ya siku ya kuzaliwa ya Matha, Michael pamoja na Bruno walikuwa wamealikwa.

Bruno aliaga mapema na kuondoka kwani haukuwa utaratibu wake kukaa maeneo ya watu wengi kwa muda mrefu, kwa kuwa Michael alikuja na pikipiki yake hakuwa na wasiwasi wowote muda wowote angeweza kurejea.

Kadri muda ulivyokuwa unaenda ndivyo Matha alizidi kunywa pombe hadi akawa hoi kabisa. Michael alikuwa amelewa kiasi cha kawaida sana, kwa pamoja waliondoka majira ya saa tano usiku kurejea nyumbani. Michael alitegemea kumfikisha Matha na kuondoka zake kuelekea nyumbani lakini haikuwa hivyo. Matha alimletea vurugu za kilevilevi hadi wakaoga wote, kama hiyo haitoshi wakaingia kitandani wote. Michael hakuweza kujizuia zaidi akakiri kuzidiwa maarifa akasalimu amri. Saa saba usiku simu ya Michael iliita, hawakuwa wamelala wawili hawa.

"Ni John!!!!" alihamaki Michael, Matha hakusema neno. Zilikuwa ni siku nne tangu aondoke na kuahidi kurejea baada ya wiki mbili.

"Niambie kaka mkubwa!!" alianza kuzungumza baada ya kupokea simu.

"Poa dogo, nishakukataza mambo ya wake za watu shauri zako hapo najua upo na mke wa mtu!!!" sauti ya John ilijibu.

"Hamna nipo kwa mwanangu mmoja hivi kanipiga pombe hatari"

"Haya bwana mi naenda kwa shemeji yako hivyo, si nilikuwa nimesahau kama leo ndo 'birthday' yake!!...yaani najua atakuwa amenuna huyo"

"Nani Matha au....eeh!! upo Mwanza" alizungumza bila kujiamini, wakati huo yule Matha aliyekuwa anajidai amelewa chakari alikuwa amekaa kitako macho yamemtoka pima.

"Ndio nipo hapa maeneo jirani na nyumba yake dakika sifuri tu nafika ndani, we endelea kulewa si ushalijua jiji mi ntafanyaje??"

Tumekwisha Matha, tumekwisha!!!! alisema Michael huku akitapatapa pale ndani. Matha naye alikuwa wima, kanga ilikuwa imedondoka na alikuwa amesalia uchi lakini hata hakulitambua hilo.

Hatia ikaunda hofu katika mioyo yao!!!



******


Katika chumba ambacho MICHAEL yupo na mpenzi wa mtu hatari kabisa....mpenzi wa JOHN MAPULU......huyu kiumbe asiyekuwa na huruma yu jirani kuingia.

MICHAEL na MATHA chumbani.....je? JOHN akiwafumania kitatokea nini...je!! ndio kifo cha MICHAEL...ama wote MICHAEL na MATHA!!!!!


ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment

Recent Posts