Friday, September 14, 2012

HATIA --- 02

Na GEORGE IRON


         Hospitali ya mkoa wa Shinyanga kwa ujumla haikuwa mbali sana kutoka mahali basi hilo la Najimunisa lilipopatia hiyo tafrani, kwa maamuzi yaliyoafikiwa na kila abiria yule binti walimzoazoa kutoka pale chini na kumweka katika siti ya mbele ambayo ilikuwa na uwezo wa kupokea watu watatu, hakuwa akitokwa na damu lakini alikuwa akigumia kwa sauti ya chini sana, mwanamke mmoja alikaa pamoja naye kwa ajili ya kumsaidia huku Michael naye akiwa karibu yake.

                                                      ******

       Hospitali ya mkoa wa Shinyanga ndio kwanza ilikuwa katika mgomo wa madaktari wakitaka mwenzao aliyewekewa zengwe na kufukuzwa kazi baada ya kushindwa kuokoa maisha ya mtoto wa Kigogo arejeshwe kazini hivyo hakuna huduma zilizokuwa zikitolewa pale licha ya madaktari kuwepo eneo hilo la Hospitali mjini Shinyanga. Kundi la wanaume wanne wakiwa wamembeba mgonjwa wao liliingia kwa uharaka wa kuhitaji huduma pale ndani, hakuna yeyote aliyewakaribisha zaidi ya ukarimu walioupata kwa mlinzi pale mlangoni huku akiwaonea huruma, kila mtu alikuwa bize sana na mambo yake binafsi yasiyoendana na mandhari ya hospitali.
“Nesi nesi…” mwanamme moja aliita lakini alijibiwa kwa jicho kali kisha mwanamama huyo akatoweka. Kwa ujasiri waliamua kujitafutia wodi mojawapo na kumlaza yule binti kitandani kisha wakaanza kuhaha kuwatafuta madaktari ambao hata hawakuonyesha kujali. Mwanzoni walikuwa wanaume wanne pamoja na mwanadada asiyejitambua hata kidogo akiwa katika maumivu makali sana ambayo hakuhitaji kujieleza mwenyewe bali jinsi alivyokuwa ameuma meno na kuikunja sura yake lilikuwa jibu tosha, baada ya muda wakabaki watatu, wawili na hatimaye mmoja Michael!! Ndio alikuwa Michael peke yake pamoja na binti.
             Nafsi ya Michael ikaingia katika mgogoro mkali, mgogoro binafsi, maamuzi yalikuwa mengi lakini hakujua lipi ni sahihi. Akiwa katika wimbi la mawazo alisikia anaguswa begani.
“Aah!! Kijana nimekutafuta kweli, ni zaidi ya saa zima sasa nilikuwa napita hapa lakini sijui kwa nini hii wodi nilikuwa naivuka.” sauti nzito kutokana na umri kwenda ilimweleza Michael ambaye alibaki kuduwaa ilikuwa mara yake ya kwanza kufika katika mkoa huu uliotawaliwa na jamii ya wasukuma halafu anatokea mtu anamfahamu.
“Mimi?.”
“Ndio wewe!!!.”
“Aaah!!! Eheee.” aliuliza Michael ili apate kujua shida ya yule mtu.
“Unawahi kusahau wewe, mimi ni yule mlinzi wa pale getini mwanangu poleni sana baba!!!! Pole sana” alijieleza yule mlinzi. Michael hakuwa na kumbukumbu kabisa kwamba pale kwenye basi walipofikia muafaka wa kumwahisha binti hospitali watu walichangachanga walichonacho na kufikisha shilingi laki mbili na nusu ambayo walimkabidhi, alipozipokea mkononi ndivyo hivyo hivyo alizishika hadi waliposhuka na kumfikia mlinzi wa geti, wakati anaandika jina lake katika kitabu cha orodha ya wageni ndio wakati huo huo aliziachia zile pesa na kuzisahau, jambo jema mlinzi huyu aliyejitambulisha kama mzee Matata aliona tukio hilo na kuokoa pesa za Michael na sasa alikuwa amempata kwa ajili ya kumpatia.
Michael alishangazwa na uaminifu aliokuwa nao babu huyu wa makamo mrefu, mwenye mwili uliojengeka na ndevu zake zilizokuwa na mvi kiasi,
“Kwa nini amenirejeshea hizi pesa??.” Alijiuliza Michael
“Asante sana mzee wangu asante sana.” Michael alijaribu kumpatia kiasi fulani cha pesa lakini mzee Matata alikataa kabisa huku akimwonea huruma Michael kwa hali aliyokuwa nayo.
“Ngoja niangalie kama utapata huduma walau ya kwanza maana huyu nani vile anaitwa??.”
“Aaah!!! Mhh!! Huyu?? Anaitwa nanii Mariam eeh!!! Mariam.” alijibu Michael kwa kujiumauma
Mzee Matata alipotoka Michael naye alifikiria kuondoka na kumwacha binti peke yake, akili ilikuwa imemruhusu lakini wakati anapiga hatua mlangoni aliisikia nafsi yake ikimtamkia neno ‘NIKO NAYE’ ambalo alilitaja pale ndani ya basi, nafsi pia ilimsuta kwa pesa aliyorejeshewa na mzee Matata, kwa kutoroka ilimaanisha kwamba amefanya dhulumati na kuweka maisha ya binti katika hatihati. Michael alizishusha pumzi zake kisha akarejea tena pale wodini kusubiria harakati za mzee Matata kama zitazaa matunda.

                                    ******
  
Akiwa ni mtoto wa tatu wa mzee Akwino Msombe ni yeye pekee aliyejaaliwa kielimu hadi hapo alipofikia, jina Michael Msombe lilikuwa maarufu sana katika shule ya sekondari Musoma Technical alipomalizia kidato cha nne kutokana na umahiri wake katika kucheza mpira wa miguu, jina hilo likaendelea kupeta katika shule za Mara Secondary na baadaye Minaki kutokana na ubora wa Michael katika suala zima la uhamasishaji wa maendeleo na kuwa mshauri bora kwa wenzake hasahasa baada ya kufanya jitihada kubwa na kuunda tawi la FEMA katika shule yake.
Katika chuo kikuu cha Dar es salaam Michael hakuwa akicheza mpira tena lakini aliendelea kuhamasisha hapa na pale lakini athari kubwa iliyopunguza uwezo wake wa kutimiza wajibu ilikuwa ni jinsia ya kike ambayo kwa mara ya kwanza alikuwa nayo karibu zaidi ya awali alipokuwa katika shule za wanaume watupu. Wasichana hawakuchelewa kutambua kitu fulani katika mwili wake, kijana aliyecheza mpira kwa kujituma miaka kadhaa iliyopita mwili wake ukiwa umejengeka vyema, mrefu wa wastani na rangi yake maji ya kunde ilimfanya aonekane mtanashati pindi anapochomekea shati lake la mikono mirefu katika suruali yake iliyopigwa pasi vyema, anapovaa jeans na fulana yake bado alionekana nadhifu, na hakuharibikia siku aliyojisikia kuvaa pensi kwani mguu wake ulistahili kuonwa na watoto wa kike.
Hayo yote yalisindikizwa na jicho hadimu sana ambalo likimtazama mwanamke atajiuliza mara mbilimbili Michael anamaanisha nini?? Maskini Michael wa watu hakuyajua hayo yeye alikuwa akihisi huenda kizuri katika mwili wake ni kishimo kidogo (dimple) katika shavu lake la kuume jambo alilojitambia tangu utotoni.
                    Akiwa na miaka 24 tu aliingia katika msukosuko wa kimapenzi wasichana wengi walimtamkia kwa midomo yao kuwa anawatesa lakini alichukulia ni utani hadi siku moja na yeye alipogundua kwamba anateswa. Ni siku ambayo alikutana na Joyce msichana ambaye walicheza naye utotoni na kisha kusoma wote shule ya msingi baada ya kumaliza shule ndipo rasmi wakapotezana baada ya Michael kuchaguliwa kujiunga Musoma tech kwa ajili ya kuendelea na kidato cha kwanza huku Joyce yeye akienda Nganza sekondari Mwanza.
Hapo chuoni walikutana mgahawani wakati Michael ananawa na Joyce anatafuta meza ya kukaa, ilikuwa ni furaha ya hali ya juu ambayo iliunda upya urafiki wao wa utoto na kuufanya wa ukubwani, kwa Joyce ilionekana kama imetosha lakini kwa Michael alitaka zaidi ya pale jambo lililomvuruga sana akili yake. Siku ya kuzaliwa kwake alitamani ibadilike kwani bila hivyo angeendelea kuumia miaka nenda miaka rudi.
“Kwanini Joy amenitenda hivi??.” alijiuliza kila siku.


                                         *****

                        Baada ya kuamua kusubiri hadi kufikia kupitiwa na usingizi Michael alikuja kushtuka binti hayupo kitandani, mbio mbio akatoka pale wodini lakini hakujua hata ni wapi anaelekea. Madaktari wote walikuwa wamenuna ni nani utamuuliza swali akupe jibu lililomaanisha ukweli, huku na huko bila mafanikio hatimaye aliamua kumuuliza daktari mmoja nadhani jibu alilopewa kama mtu akiwa katika hali ya kawaida anaweza kutenda dhambi.
“Samahani kaka si una namba yake huyo mgonjwa hebu mpigie umuulize yuko wapi.” sauti ya kike ilimjibu Michael donge zito la hasira likambana, ili kuliondoa akajisogeza ukutani akaruhusu machozi yamdondoke, alidhani yatatoka kidogo lakini yalimwagika mengi huku kwikwi nayo ikichukua nafasi yake.
“Nchi yangu Tanzania…yaani mimi nimpigie mgonjwa simu aaah!!!.” alilaumu huku akijigongagonga kifua chake.


                                                  *****

                       Kutoonekana kwa binti na majibu mabovu aliyopewa na yule nesi yalimtia hasira sana Michael, ni mzee Msombe pekee aliyekuwa na uwezo wa kumtambua Michael (mwanaye) wakati anakuwa na hasira na si mwingine, Michael alitamani kumvaa yule nesi na kumchapa vibao lakini nafsi ikamsihi awe mtulivu. Kama vile mwendawazimu ama mtu aliyepoteza kitu cha thamani na sasa anakitafuta kwa udi na uvumba ndivyo ilivyokuwa kwa Michael alizurura pande tofautitofauti hadi akakata tamaa na kukaa chini bila kujua kama amekaa chini tena mbele ya mlango wa kuingilia chumba cha upasuaji.
“Oya vipi wewe mbona umeziba njia??.” swali hilo ndilo lilimshtua na kutoka pale mara moja, wakati anaondoka hakuacha kuangaza huku na huko kama kuna uwezekano wa kumwona binti, pesa iliyokuwa mfukoni mwake ndio iliyomnyima amani laiti kama asingekuwa na ile pesa aliyochangiwa kwa ajili ya matibabu ya yule binti basi huenda angekuwa ametokomea tayari, lakini hata kama asingekuwa na hiyo pesa kauli iliyotoka katika kinywa chake bado ilimfunga ‘NIPO NAYE’…… “Hata!!!! Huyu ni ndugu yangu siwezi kumuacha!!!!” alijikuta akisema kwa sauti ya juu kijana huyu.
“Vipi tena mjukuu wangu mbona upo hapa??? Kwani kuna mkeo hapa ndani amejifungua!!” alipokea swali hilo Michael huku akijipatia jibu lake kwa kutazama maandishi yaliyoandikwa mlangoni ‘Wodi ya wazazi’
“Aaaah!! Mzee ni wewe, simuoni mgonjwa wangu mzee wangu.” alikuwa ni yule mlinzi aliyeiokota pesa na kumpatia Michael
“Haaa!!!! Ina maana wakati tunamtoa pale wewe ulikuwa umelala, basi una usingizi mbaya.”
“Mlimtoa wapi?? Saa ngapi??...eeeh!! mzee wangu.” aliuliza kwa wasiwasi.
“Kumbe kweli ulikuwa unaota..yaani umetuambia kabisa tutangulie we tutakukuta mh!! Hebu tuachane na hayo…yule sijui mkeo ame…”
“Aaah!!! Babu si mke wangu yule bwana” alikanusha kwa aibu aibu Michael
“Yote sawa….kama nilivyokuhaidi nilimpata rafiki yangu mmoja hivi ni Daktari alinisaidia tukambeba hadi katika chumba kimoja hapo juu akampatia huduma ya kwanza kwa siri sana wenzake wasigundue……”
“Ana tatizo gani?? Amepona???” aliingilia kati Michael
“Tulia mjukuu wangu….yule binti ulisema sijui Maria eeh!!”
“Eeh!! Maria anaitwa Maria.”
“Tatizo alilonalo si kubwa sana lakini ni kubwa kwa upande mwingine…alishtuka kiuno”…(Michael akakunja uso kwa uchungu)
Mzee akaendelea.. “Ilibaki kidogo tu avunjike jumla lakini daktari amejaribu na kukirudisha mahali pake..kinachotakiwa sasa ni mazoezi ili azoee hiyo hali na kurejea kuwa mzima tena” alimaliza
           “Sasa ina maana hayo mazoezi anafanya kwa siku ngapi…asante sana babu”
“Anafanya kwa siku kumi na nne kama asipokuwa mzembe anapona hata kwa siku kumi” alielekeza yule babu
“Yule sio mzembe mi namfahamu sana” alidanganya, kwani hata alikuwa hajawahi kuzungumza naye huyo binti na kama hiyo haitoshi hata jina alikuwa hamfahamu
“Haya sasa itambidi kesho afanye mazoezi halafu…..mh!!! una sehemu ya kuishi hapa Shinyanga au upo gesti??” mzee huyo mrefu mwenye lafudhi ya kisukuma alimuuliza Michael.
“Kwa kweli mimi hapa ni mgeni sio siri nilikuwa naelekea naye Mwanza huko ndo nina wenyeji babu” alijieleza kwa upole sana Michael.
“Hamna shaka nitazungumza tena na daktari yule rafiki yangu aangalie uwezekano wa kukupatia chumba mgonjwa awe anapumzika wewe utakuwa unalala gesti nadhani itakusaidia”
“Yaani sana mzee wangu nashukuru kwa wema wako..”
“Usijali hata mimi nina wanangu wanasoma huko Arusha na Manyara, nisipotenda wema kwa watoto kama nyie na wangu mimi nani atawatendea wema???”

                                                                           ******

                          Joyce alishikwa na butwaa kali sana, si kwa sababu alimwona Michael alivyowafumania akiwa uchi wa mnyama na mwanaume mwingine ila ni kwa jinsi Joyce alivyowahi kumueleza Michael wakati wapo chuoni kwamba alikuwa akimchukia sana yule mwanaume ambaye leo hii amefumaniwa naye.
“Mama yangu!!! Nitauficha wapi uso wangu mimi na tunaenda kufanya kazi sehemu moja dah!!!” alijiuliza bila kupata majibu. Hofu ilimtawala akashindwa hata kupiga namba za simu za Michael kwa kuhofia kuzidi kumkwaza.
                       Michael hakuwa na mahusiano ya kimapenzi na Joyce binti wa miaka ishirini na nne mtoto wa mwisho wa mfanyabiashara ya mitumba Stanley Keto, lakini ilikuwa kazi rahisi kuhisi watu hawa walikuwa na mahusiano ni wao pekee walilijua jibu sahihi la fumbo hilo. Michael na Joyce walikuwa wanatamaniana lakini hakuna aliyemuanza mwenzake, hali hiyo ikamfanya Joyce aamini, kwa jinsi Michael alivyokuwa akiwavutia wasichana basi lazima atakuwa na mahusiano na msichana flani hapo chuoni.
                    Hisia zake hizo zikamsukumia na yeye kuamua kujivinjari na mwanaume mwingine, kwa muda mrefu alikuwa hajamkubalia Victor Nicholaus katika suala zima la tendo la ndoa lakini katika siku kuu ya kuzaliwa Michael Msombe akajikuta amemruhusu kaka huyo kuutawala mwili wake na ni katika siku hiyo Michael kwa macho yake anawafumania.
Joyce alijua ni jinsi gani Michael aliumizwa na kitendo kile. Kosa kubwa alilofanya ni kukaa kimya kwa siku mbili akiamini hasira za Michael zitakuwa zimepoa, siku ya tatu Michael hakuwepo tena katika viunga vya jiji la Dar es salaam na hakujua ni wapi alipoelekea nani angemwelekeza!!!. Alivuta subira hadi muda wa kufanya field ulipofika lakini hiyo haikuwa suluhisho Michael hakuonekana na simu yake haikuwa ikipatikana.
“Atakuwa ameweka ile namba nyingine lakini nayo sikuwahi kuichukua” hakuwa na ujanja mwingine Joyce kwani kwa marafiki pote hapakuwa na jibu la kuridhisha

                                                                               ******
                 Siku tisa pekee zilitosha kwa binti kupona kabisa kiuno chake, ilibaki michubuko kadhaa tu katika paji la uso na mikononi lakini haikuwa na madhara makubwa sana.
“Mkeo ni jasiri sana!!!!” daktari alimsifia Michael wakati anamuelezea jinsi yule binti waliyemtambua kwa jina la Maria alivyopona upesi. Michael alicheka kwa kujilazimisha, moyoni alikuwa anahofia kuhusu suala la pesa maana katika akaunti yake pesa ya field ilikuwa haijaingia bado, na mfukoni alikuwa na shilingi elfu hamsini pekee na alijua ni lazima amlipe yule daktari, kwa kuwa alikuwa amezoeana na yule babu alimvuta pembeni kwa ishara kisha akamueleza kuhusu hilo tatizo lakini hata kabla hajamaliza mzee akaingilia kati
“Michael mjukuu wangu mimi nimekusaidia kwa vyote hivyo ile ishirini uliyotoa kwa ajili ya dawa imetosha sana….”
“Aah!! Babu kweli!!!”
“Ndio wewe usijali…vipi safari lini sasa au tuko pamoja bado…umeionaje Shinyanga kwanza”
“Shinyanga ni nzuri na mnaipendezesha wema kama nyie..kesho asubuhi nitadamka mapema na kuwahi gari za awali sana”
“Ukipita Shinyanga usikose kuja kunisalimia” baada ya maongezi ikiwa saa sita mchana aliwaaga na kuwashukuru daktari na mzee Matata kisha akamchukua yule binti na kuondoka naye kwa mwendo wa taratibu.
“Unajisikiaje??”
“Nafuu sana asante Michael”
“Nani amekwambia naitwa Michael”
“Mzee Matata na daktari..”
“Wamekudanganya!!”alijibu kwa ufupi Michael.
                           Saa moja usiku Michael na binti walikuwa chumbani Michael hakuwa muongeaji sana licha ya binti kujisemesha kila mara, hata jina pekee bado Michael alikuwa hajamuuliza. Tayari Michael alikuwa ameoga wakati huo binti akiwa nje hadi alipomaliza kuvaa ndo akamruhusu na yeye aingie kuoga wakati yeye (Michael) akatoka nje. Michael alitembea huku na huko bila sababu ilimradi binti amalize kuoga na kuvaa wapate kulala.
“Nikirejea nampiga maswali kisha nampa nauli aende anapojua yeye.” Alijisemea wakati huo dakika ishirini zilikuwa zimepita.
“Mh!! Hamalizi tu kuoga wanawake nao.” akiwa ametoka dukani kumnunulia binti mswaki alijisemea hivyo baada ya kuona kimya kikali kikiendelea.
Simu ya mkononi ya Michael iliita, kumbe alikuwa ameisahau ndani ya chumba, hiyo ndiyo ilimlazimu kushusha kitasa chini na kuuruhusu mlango ufunguke haraka haraka akaingia ndani. Almanusura apoteze fahamu aliyatumbua macho yake, mdomo ukabaki wazi lakini sauti haikutoka, baridi kali ikaukumba mwili wake, miguu ikaanza kuishiwa nguvu hakuamini kilichokuwa kinatokea.
Alisahau kwamba ni mlio wa simu yake uliomlazimu kurejea ndani bila kuruhusiwa na yule binti. Marumaru nyeupe iliyokuwa chumbani hapo ilikuwa imechanganyikana na wekundu, mwili wa binti ulikuwa uchi juu hadi maeneo ya mapajani, hakufanya maksudi kuwa katika hali ile lakini alikuwa hajitambui tena.
                               Binti alikuwa amezirai, Michael alibaki amezubaa asijue wapi pa kuanzia, hakuchelewa sana kugundua chanzo baada ya akili yake kukaa sawa, binti alikuwa ameteleza wakati anatoka bafuni na kuanguka chini vibaya, Michael hakuweza kukisikia kishindo hicho kwani alikuwa ametoka mbali kidogo na eneo la mlango wa kuingilia chumbani hapo.
“Binti!!!...binti!!!! we dada….” Aliita huku akijaribu kumtikisa kidogokidogo, hakupata jawabu lolote lile.

NINI KIMEMSIBU…..
Endelea nayo jumatatu ijayo

1 comment:

Recent Posts