Wednesday, September 19, 2012

HATIA---04


Na GEORGE IRON

Dakika tano ziliwatosha kumpekua Michael na kufanikiwa kukutana na pesa kidogo tu kama shilingi elfu ishirini, badala ya kufurahia kidogo kilichopatikana bila jasho lao walipandwa na hasira.
“Pesa zipo wapi????.” lilikuwa swali moja zito sana kwa Michael hakufahamu hawa watu wamejuaje kuwa ameingiziwa pesa za mkopo katika akaunti yake ndani ya dakika chache zilizopita.
“Nakuuliza wewe pesa ziko wapi????” hakuwa na cha kujibu Michael, pigo jingine la nguvu katika mgongo wake, akajikunja kwa uchungu kisha akajikunjua baada ya kugundua ameegemea sana katika mdomo ambao risasi hupitia kwenye bunduki iliyokuwa jirani na shingo yake.
“Sina pesa mimi jamani ni mwanafunzi…..mimi mwanafunzi jamani…” alijitetea wakati huo Joy yeye yupo kimya. Jibu hilo lilikuwa karaha kwa watu hawa wabaya, waliendelea kumpiga Michael kwa awamu huku kwa maksudi wakiwa wameifungulia luninga iliyokuwa hapo ndani sauti ya juu hivyo mtu wa nje hakuweza kusikia kinachoendelea. Kadri jinsi Michael alivyojitetea ndivyo majambazi hawa walianza kupatwa na wasiwasi huenda wanamuhukumu mtu ambaye si sahihi
“Kocha….una uhakika ni chumba namba 18……mbona humu tumekuta mwanafunzi!!!.....” Mawasiliano hayo kidogo yakafufua ndoto za Michael na Joy kupona dhidi ya watu hawa.

****
Jitihada za Joyce Keto jijini Dar es salaam kumpata Michael hazikuzaa matunda, pale nyumbani alipokuwa akiishi Michael walidai kuwa aliondoka ghafla na hawafahamu alipo japo si mara ya kwanza kufanya hivyo. Rafiki zake Michael walimuelezea kwamba alikuwa katika hali ya unyonge sana kabla ya kutoweka bila kuaga. Majibu hayo yalimtia mashaka sana Joyce, aliogopa sana kuwaambia watu ukweli juu ya nini kilichotokea walipoonana na Michael kwa mara ya mwisho.
Michael alikuwa amemfumania akiwa na mwanaume mwingine!! Hilo ndilo jambo aliloamini kuwa limesababisha kutoweka kwa Michael katika mazingira ya kutatanisha.
“Lakini mimi sikuwahi kuwa na uhusiano na Michael licha ya watu wengi sana kuhisi mimi na yeye ni wapenzi.” aliwaza na kuwazua Joyce Keto. Ina maana alichukulia serious watu walipotuita wapendanao!! Alijiuliza. Aliogopa sana kumshirikisha mtu yeyote juu ya uhusiano wa kutoweka kwa Michael na tukio la kufumaniwa kwake. Kichwa kilimuuma sana kila alipojaribu kumpigia simu Michael na kuendelea kupata jibu lile lile kwamba namba anayopiga haipatikani.
“Kama amejiua je???.” ghafla wazo hilo liliiteka akili ya Joyce. Mh!! Mtihani!! Alihitimisha mawazo yake kwa kupanda gari na kuelekea chuoni, foleni kubwa barabarani ilimtia hasira. “ah!! Elfu tatu kitu gani bwana.” alijisemea huku akiomba kushuka kisha akakwea bajaji, ghadhabu yake ikapungua kidogo kutokana na kupata hewa ya kutosha. Dakika kadhaa zilitoweka Bajaji ikawasili katika viunga vya chuo. Joyce akashuka na kulipa pesa, kisha hatua kwa hatua akajikongoja taratibu hadi mbele ya ofisi alizokuwa amepanga kwenda.
“Nimejaza namba ya simu ambayo si sahihi!!.” alijieleza Joyce mbele ya mkuu wa kitengo hicho.
“Bwana eeh!! Mmezidi na nyie haya chukua uangalie mwenyewe wino wa kufutia huo hapo utajirekebishia, yaani watu wazima tunakuwa kama shule ya chekechea ah!!!” alizungumza kwa hasira mwanamke aliyekuwa katika kitengo hicho. Kwa Joyce huo ulikuwa ushindi mkubwa sana, ni jambo lililompeleka.
“Huku wasichana huko wavulana” maelezo tosha kabisa kwa Joyce. Haraka haraka alianza kupekua katika majina ya wanaume 1…2….3….4….5…..alizihesabu namba hadi akafikia thelathini na tatu ‘Michael Msombe’!! moyo ulimpasuka na kumuongezea hamu ya kujua kilichoandikwa mbele yake, Mugumu Serengeti!! Ndio wapi sasa huku!!! Alijiuliza Joyce huku akirudia mara mbilimbili kulisoma jina hilo bila dalili yoyote ya kuliweka akilini mwake ipasavyo.
Mkoa wa Mara!! Msamiati mwingine tena. Ili kuhifadhi kumbukumbu hiyo aliamua kuitumia simu yake kuandika kila alichoona ni kigumu kumeza kwa haraka haraka.
“Michael ameenda wapi huku…hivi ni Tanzania…” alijiuliza Joyce.
“Hivi wewe, mbona mzembe hivyo humalizi tu!! Unaboa bwana.” alilaumu yule mama aliyempa Joyce faili kwa ajili ya kufanya marekebisho.
“Ah!! Samahani na ikiwa unataka kuhamishwa sehemu ya kufanya field unafuata process gani???” badala ya kujibu aliuliza swali jingine Joyce na kumtia hasira yule mama.
“Hebu nipishe hapa ushanitia hasira….toka toka toka…tafadhali!” Joyce hakutaka shari huyoo akajiondokea, aliona nyumbani ni mbali sana akiwa ndani ya daladala alifungua simu yake katika sehemu ya internet akaenda google kisha akatafuta google map na kuandika Mugumu Serengeti, ilichukua sekunde kadhaa kutoa jawabu kwamba haikufanikiwa kupakua (load).
Simu ya Joy haikuwa na salio la kutosha. Kompyuta yake ndogo nyumbani ilitumia sekunde chache ikaleta majibu ya kuridhisha.
“Michael ndo ameenda huku kweli ama amelaghai pale ili nisifahamu alipoelekea??” kabla hajapata jawabu simu yake ya mkononi iliita, ilikuwa namba mpya kwake.
“Haloo!!.” aliita


“Haujambo mwanangu!!!.”
“Sijambo, nani??” aliuliza Joyce
“Mama yake Michael….” Moyo ulimpasuka Joyce kama vile amepigwa shoti ya umeme alitulia tuli
“Shikamoo mama….shikamoo.”
“Marahaba Joy, za siku nyingi mwanangu??”
“Ni nzuri mama, sijui nyie.”
“Sisi wazima kidogo, lakini huyo mwenzako hata kwenye simu hatumpati kulikoni.” aliuliza mama yake na Michael kwa sauti iliyosawazika.Kimya kilidumu kwa sekunde kisha Joyce naye akaelezea kutompata kwake hewani.
“Nadhani yatakuwa matatizo ya simu yake, nitaenda kwake kumuarifu kuwa unamtafuta” alisema tu kumridhisha mama huyo lakini ukweli ni kwamba Michael hakuwepo. Kwa jinsi Michael alivyomueleza Joyce juu ya uhusiano wake mzuri na mama yake tangu akiwa mtoto mdogo aliyetelekezwa na baba yake mzazi, Joyce aligundua kuna tatizo linataka kuibuka tena tatizo kubwa sana.
“Lazima nifanye kitu mimi ndiye chanzo cha haya yote.” alijishauri.
“Hivi kwani alinitambulishaje kwa mama yake!!!!.....nipo hatiani Joyce mimi”

BAADA YA SIKU TATU

Joyce Keto kwa ujasiri wa hali ya juu baada ya kuwa amemaliza hatua zote za kuhama sehemu ya kufanyia field na kuwa Serengeti Mugumu, alikuwa ndani ya gari akielekea katika mkoa asioufahamu hata kidogo, lengo likiwa kujitoa katika kitanzi cha hatia inayomkabili. Mama yake Michael ndiye alimuumiza sana kwani Michael alikuwa ndiye mtoto wake wa pekee aliyezaa na mzee Msombe kabla ya kutelekezwa na kisha mzee Msombe naye kupotea ghafla katika mazingira ya kutatanisha. Michael ndiye faraja pekee iliyokuwa imebaki katika dunia ya mama yake.
Kama amekufa itakuwaje!! Eeh!! Mungu muepushe!! Aliomba Joyce wakati safari inaendelea.

****

Matumaini waliyoyapata Joy na Michael kuwa huenda wale watu watawaacha kwa kugundua si watu sahihi hayakuwa sawa hata kidogo, kwani waliendelea kuulizwa maswali ambayo majibu yake yalikuwa magumu mno. Baada ya Michael kubanwa maswali huku akipokea kipigo hatimaye aliwakubalia kwamba ana pesa kiasi lakini katika akaunti yake.
“Tunaongozana hadi hapo ATM, ole wako upige kelele aina yoyote ile mara moja nausambaza ubongo wako na wewe kuku hapo kitandani tulia hivyo hivyo nadhani unajua madhara ya kupiga kelele.” alifoka jambazi mmoja huku akimalizana na Michael na kumgeukia Joy.
“Weziiiiii……weziiiiiiiii..tusaidieniiiiii” Joy alipiga kelele ghafla baada ya umeme kuwa umekatika na kusababisha ukimya pale ndani, sauti yake ilimshtua kila mtu hata Michael alishindwa kuelewa ni wapi Joy ameutoa ujasiri huu, baada ya hizo kelele kimya kikuu kilifuata baada ya mshindo kusikika.

****
Kituo kikuu cha polisi Mwanza, chumba cha mahabusu kilikuwa kimejaa sana lakini bado wengine waliendelea kuongezwa, kelele za mahabusu hazikuwakera polisi waliozidi kutoa amri kwa watuhumiwa waliokamatwa kuvua mkanda, saa, viatu na kuingia mahabusu. Majira ya saa mbili usiku aliingizwa mtuhumiwa mwingine
“Mapulu!!! Mpeleke chooni huyo” sauti kali ya afande iliamuru. Mapulu alikuwa ni mahabusu aliyekaa siku nyingi sana katika kituo hicho, alikuwa na muda wa mwezi mzima hivyo alikuwa ni mzoefu sana na alitokea kuitwa ‘faza hausi’, huyo ndiye aliyewapokea mahabusu wapya na alizifahamu taratibu zote za hapo ndani. Alikuwa ni mjelajela kweli kwani haikuwa mara yake kufungwa na kuhusu kutiwa mahabusu ilikuwa ni kama kamchezo flani hivi hakuwa na hofu.
Mahabusu aliyeingia alikuwa akilia kama mtoto mdogo licha ya umbo lake kuonyesha ujasiri wa hali ya juu.
“Pumbavu!! Unamlilia nani hapa unadhani kwa mamako hapa, kuja huku nikupe chumba!!!” John Mapulu alimkaripia huyo mgeni huku akimzaba kibao katika mgongo wake, Mapulu alipokelewa na mahabusu wengine waliogundua kwamba huyo mgeni alikuwa dhaifu sana na ilikuwa mara yake ya kwanza kuingia mahabusu.
Moja kwa moja alipelekwa bila kupinga katika mlango wa choo, harufu iliyompokea kuanzia mbali alitamani sana ardhi ifunguke ajitie humo ndani milele lakini hiyo ilikuwa ndoto ya linacha.
“Umefanya nini mpaka umeletwa hapa ndani??” aliulizwa
“Sijui hata!!!.” alijibu
“Hujui!!! Kwa hiyo wamekuchukua tu…au huna sehemu ya kulala wamekupa hifadhi kwa leo???.” aliulizwa tena kwa kuzodolewa. Hakujibu kitu!.
Hakika ilikuwa mara yake ya kwanza kuingia katika sehemu hiyo lazima ajisikie mpweke. Usingizi hakujua ataupatia wapi kutokana na ile harufu lakini alishangaa alipoamshwa asubuhi kwa kukanyagwa kanyagwa na watu waliokuwa wakielekea chooni, usingizi ulimpitia bila kujua.
“Amka usafishe choo!!!!” aliamriwa na kijana ambaye laiti kama wangekuwa nje ya selo hiyo angeweza kumuita ‘dogo’ lakini nyuma ya chuma hizo hakuwa na ujanja alisimama na kufanya kama alivyoelekezwa mwili mzima ulikuwa unanuka!!
“Michael msombe!!!” sauti ya afande iliita, lilikuwa jina geni pale ndani kila mtu akaanza kumuangalia mwenzake.
“Michael!!” ilirudia sauti ile kwa ukali
“Naam!!!!” ilisikika sauti kutokea chooni
“John!! We mtu mbaya sana kumbe umemlaza chooni kweli” afande alisema kwa utani baada ya kumsikia aliyemuita akiita kutokea chooni.
Suruali yake ya jinsi ilikuwa inamtelemka kutokana na kukosa mkanda wa kuikamata, macho yake yalikuwa yamevimba kwa kutokwa machozi sana huyu alikuwa ni Michael Msombe.
Si kweli kwamba hakujua kwanini yuko pale ila ni uoga tu wa kuingia selo kwa mara ya kwanza ulimtetemesha. Michael alikuwa anatuhumiwa kwa kesi ya mauaji ya mtoto wa kike katika guest ya Double G jijini Mwanza. Kesi ambayo kwa asilimia kubwa haikuwa na ushahidi wa kumfunga lakini alikuwa ndani kwa ajili ya upelelezi, hakuwepo mtu anayemshtaki Michael tofauti na jamuhuri ya muungano ya Tanzania.
“Huna ndugu yako umpigie aje akuwekee dhamana??” aliulizwa Michael baada ya kulifikia geti la chuma lililokuwa limefungwa imara.
“Nilikuwa nasafiri!!!.”
“Pumbavu, sijakuuliza kama ulikuwa unasafiri ama la..nimekuuliza una ndugu we fala nini??” alifoka askari, Michael akakosa cha kusema.
“Mpuuzi wewe, nakuuliza unadengua unadhani mi nakutongoza au??? Haya utaozea humu ndani” maneno hayo ya afande yaliugalagaza vibaya moyo wa Michael, hakuwa na hatia lakini alinyanyasika. Michael alikuwa ameikariri vizuri namba ya mama yake mzazi lakini aliamini kuwa kwa kuruhusu mama yake apigiwe simu ilikuwa ni tiketi sahihi ya kumruhusu mama huyo mjane aitenge roho yake na dunia hii, mara chache sana Michael aliacha kujutia kitendo cha kumsaidia Joyce katika safari waliyokutana, Joy ameharibu mipango yangu yote!! Aliwaza lakini akayapinga mawazo yake baada ya kukumbuka huyo Joy anayemzungumzia yeye sasa ni marehemu si hai tena
“0717..7….3…76..12” aliitaja namba hiyo kwa askari wa zamu ambaye kidogo alikuwa mstaarabu.
“Haya nitampigia….”
“Tafadhali mwambie asimwambie mama” afande hakujibu akajiondokea. Zilikuwa ni siku tatu tangu atiwe selo, hata siku moja hakuwahi kupelekwa mahakamani kisa ushahidi haujakamilika.
Mazingira ya selo yalikuwa magumu sana kuzoeleka kwa upande wake, japo alikuwa ameanza kupata marafiki ambao walikuwa wakimkaribisha chakula aliamini hapo si mahali sahihi kwake yeye, bado elimu yake ilimtia ushawishi kwamba watu wenye elimu hawatakiwi mahali pale.
“Mbona sasa hawa wasio na elimu wameninyanyasa, lakini hata sikuulizwa nina elimu gani wakati naingizwa hapa ndani, kweli wanajali elimu hapa!!!! Hapana sidhani” alipata jawabu na kuanzia siku hiyo akaifuta dhana hiyo. Siku ikapita bila kumwona tena yule afande, wakati huu alikuwa halali tena kule chooni bali walilala wale wageni.
Zilikuwa zimepita siku sita tangu Michael aingizwe pale ndani, walikuwa wanaingia wengine na kutoka lakini yeye hakuwahi kuja kutembelewa na ndugu yeyote yule. Ilifikia wakati baada ya John Mapulu ni yeye aliyekuwa anafuata kwa uzoefu pale ndani.
“Hivi wewe huna ndugu!!!” John alimuuliza Michael siku hiyo wakiwa wanakula ugali na maharage ulioletwa kwa ajili ya mahabusu.

“Ninao ila wako mbali.”
“Huwa namsikia afande anasema uliua, je ni kweli??.”
“Hapana kaka sikuua ila, kuna binti nilikuwa naye……” Michael alisimulia kila kitu jinsi alivyokutana na Joyce katika basi, maswahibu waliyoyapata Shinyanga na makubwa zaidi yaliyochukua uhai wa Joy hapo Mwanza. Michael alielezea kitendo cha Joy kupiga kelele kilivyowatia hasira majambazi na kufikia hatua ya kumpiga hadi kumuua.
“Wewe sasa umekamatwaje??.”
“Baada ya Joy kuwa ameuwawa niliwataarifu mapokezi, wao wakapiga simu polisi. Polisi walichelewa kuja lakini baadaye walikuja, walimchunguza Joy kwa macho kisha wakamwacha kama alivyo, kesho yake walikuja na daktari akamfanyia uchunguzi sijui alitoa majibu gani, baada ya siku mbili nikiwa mtaani nilipigiwa simu na watu nisiowafahamu….”
“Ukawaeleza ulipo wakaja kukukamata…” alimalizia John kuonyesha kwamba anayajua sana mambo hayo.
“Ni kweli na walinikamata kwa shari sana, walinipiga na kunitia pingu.” alimalizia Michael.
“Ulifanya kosa kubwa sana kuwasubiri, baada ya tukio usingebaki…hawana dogo hawa wanapenda sana………mh!!! Umeandikisha shilingi ngapi katika PPR yako??”
“PPR?? Ndo nini.” aliuliza Michael
“Kikaratasi kilichoandikwa vitu ulivyoacha hapo kaunta”
“Aah!! Elfu tatu”
“Elfu tatu?? Hawakuachii hawa” alihamaki Mapulu. Michael akasononeka waziwazi na kukata tamaa. John akainuka na kuelekea katika chumba kingine.

*****


ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment

Recent Posts