Friday, September 21, 2012

HATIA--05


Na George Iron

MUGUMU SERENGETI

Usumbufu aliokuwa akiupata kutoka kwa mama yake Michael kuhusu mwanaye ulimkosesha amani Joyce Keto sasa alikuwa ameeamua kubadili laini ya simu yake ili aweze kuwa na amani walau kiduchu. Mara moja moja alikuwa akiiweka ile laini na kusoma baadhi ya jumbe zilizokuwa zimeingia kisha kuitoa katika simu.
“Mwenye namba 0657727324 amekupigia simu saa……” ulisomeka ujumbe katika simu yake.
“Mh!! Atakuwa nani huyu jamani…” alijiuliza Joyce akiwa katika kitanda chake katika nyumba aliyopanga kwa muda. Haraka haraka alizinakiri zile tarakimu katika karatasi na kisha akatumia simu yake nyingine kupiga.
“Hallow!!” upande wa pili ulipokea ilikuwa sauti nzito ya kiume.
“Samahani kaka, nimekuta ujumbe wako kwamba ulinipigia simu lakini sikuwa napatikana” alijieleza Joyce
“Hii simu wanatumia watu wengi, afande Matiko Mwanza hapa je kuna uhusiano wowote” aliuliza
“Ahh!!! Sijaelewa.”
“Labda kuna ndugu yako ni mahabusu maana hawa ndio wanapiga piga simu sana kwa ndugu zao, kwani hiyo namba yako ni ipi” aliuliza na Joy akamtajia naye akawa anaiandika.
“Aaaah!! Kuna ndugu yako huku tena ana siku nyingi sana anaitwa Michael Msombe” alijieleza yule afande.
“Nani Michael????......upo wapi afande wewe, kwani amefanya nini tena…aah!!! Umesema Mwanza” alijikanyaga kanyaga Joyce baada ya kupokea taarifa hiyo.
“Mwanza kituo kikuu cha polisi…usiku mwema” aliaga na kukata simu.
Bila kuchukua ruhusa kazini, siku iliyofuata Joyce alidamka mapema sana na kupanda mabasi yaendayo Mwanza, ni mwendo wa masaa manne hadi matano kulifikia jiji la Mwanza. Siku hii aliiweka hewani ile namba yake ya siku zote na tayari alikuwa amempigia mama yake Michael na kumweleza kuwa Michael yupo Mwanza na anakwenda kuonana naye.
“Mwambie anipigie kuna tatizo huku sawa mwanangu, asante eeh!!” alijibu mama yake Michael kwa furaha.
Safari ilikuwa ndefu sana lakini hatimaye wakalifikia jiji la Mwanza hii ni baada ya kupanda mabasi mawili kwani basi la moja kwa moja halikuwepo siku hiyo.
“Naitwa Joyce Keto….natokea….”
“Sema shida yako…” alikatishwa na polisi aliyekuwa kaunta
“Kuna ndugu yangu hapa anaitwa Michael Msombe nimekuja kumwona nasikia amekamatwa”
“Anaitwa nani na amekamatwa lini???” aliuliza kwa hofu afande
“Sifahamu….”
“Haya subiri hapa dakika mbili…. Una uhakika wewe ni ndugu yake” alihoji Joy akatikisa kichwa kuashiria kukubali
“Hakuna mtu kama huyo hapa” lilikuwa jibu la afande.
“Hapa ndio central….” Aliuliza Joyce
“Ndio hapa kwani hujui kusoma” alijibiwa kwa mkato na yule afande ambaye alionyesha kuwa hakupenda kuzungumza na Joyce.

****

Taratibu Michael na John Mapulu wakawa marafiki ndani ya lock up, mara kwa mara walipiga stori za hapa na pale kuhusiana na maisha halisi huku simulizi za John zikimsisimua sana Michael ambaye hakuwa na jambo lolote lile la kutisha nje ya chuma hizo za mahabusu.
“Mimi ni mbaya naua dakika yoyote ile kisha nasahau!!!!” alisisitiza John na kumwacha Michael mdomo wazi akiwa haamini kama yupo karibu na mtu wa hatari kiasi kile, japokuwa John hakuwa na mwili uliojaa sana lakini alikuwa na makovu mengi sana kuonyesha kwamba amebobea.
“John Mapulu!!!!!” iliita sauti ya afande aliyekuwa ameikaza sura yake kana kwamba analinda mahabusu hata mmoja asitoroke, huku John akiamini sauti hiyo ilikuwa ni ishara kwamba mahabusu mpya ameingia hivyo aje kumpokea la! Haikuwa hivyo John baada ya siku nyingi alihitajika nje ya selo hiyo, labda kwa ajili ya mahojiano!!!, labda kupelekwa mahakamani, au kuachiwa huru kabisa!!! Hapana haiwezekani kwa muharifu kama huyu.
“Dogo kama nisiporudi mamlaka yote sasa juu yako, naweza kuwa napelekwa sehemu inaitwa ‘Sitaki maelezo’ huko ni hatari sana mdogo wangu hakuna mwanaume hata mmoja anayeweza kusita kutoa machozi, wanatesa vibaya sana na bila kujali lolote unaweza ukafa na usishtue jamii, na ujasiri wangu wote kule napaogopa sana, ukifanikiwa kutoka salama wewe si mwanaume tena!! Kule wananyanyaswa wenye makosa na wasio na makosa, hakuna huruma kule” kwa mara ya kwanza Michael akaisoma hofu aliyokuwa nayo John baada ya kuhitajika nje ya selo hiyo.
Michael hakuwa na la kuongezea, moyo wake ulidunda mara mbili ya mwendo wa kawaida huko Sitaki maelezo aliwahi kupasikia tu kuwa ni kituo cha polisi cha Mkuyuni lakini maalumu kwa ajili ya mahojiano na watuhumiwa wa makosa ya jinai. Mh!! Hivi na mimi nina kosa la jinai eeh!!! Alijiuliza Michael na kuzidi kupatwa hofu.
“John!!! Nakusubiri wewe!!!” alizidi kusisitiza afande, kwa unyonge John akaiangalia selo na kutoka nje, suruali aliyoivaa haikuwa na uwezo wa kukaa kiunoni. Alikuwa amekonda sana!!
Michael alibaki mkiwa japo hakuna aliyethubutu kumsumbua kwa lolote amani haikuwepo nafsini mwake, huku akiwa anaamini fika kuwa John Mapulu hatarejea, muda wa saa tatu usiku akiwa amelaa baada ya kuwa wamehesabiwa alimsikia John akirudishwa pale mahabusu.
“Kwa kesi niliyonayo sasa hivi wataninyonga!!! Sipo tayari kufa kwa sasa” ni maneno ya kwanza kabisa John kumnong’oneza Michael ambaye alikaa kitako kumsikiliza vyema.
“Kwanini kaka unasema hivyo na imekuwaje umerudishwa hapa ndani??” alihoji Michael kwa mtindo uleule wa kunong’oneza.
“Nitakueleza lakini kwa sasa hebu ngoja….watu wote wamelala hapa ndani??.”
“Nahisi watakuwa wamelala ni muda mrefu sana tangu waache kuzungumza” alipojibiwa hivyo aliingiza mkono wake mmoja sehemu zake za siri na kuibuka na kitu ambacho Michael hakukifahamu si tu kutokana na giza hapana hakuwahi kukiona kabla.
“Dogo umewahi hata siku moja kufikiria kuwa maisha yako yanaweza kuishia gerezani??.”
“Hapana kwani vipi??.”

Wednesday, September 19, 2012

HATIA---04


Na GEORGE IRON

Dakika tano ziliwatosha kumpekua Michael na kufanikiwa kukutana na pesa kidogo tu kama shilingi elfu ishirini, badala ya kufurahia kidogo kilichopatikana bila jasho lao walipandwa na hasira.
“Pesa zipo wapi????.” lilikuwa swali moja zito sana kwa Michael hakufahamu hawa watu wamejuaje kuwa ameingiziwa pesa za mkopo katika akaunti yake ndani ya dakika chache zilizopita.
“Nakuuliza wewe pesa ziko wapi????” hakuwa na cha kujibu Michael, pigo jingine la nguvu katika mgongo wake, akajikunja kwa uchungu kisha akajikunjua baada ya kugundua ameegemea sana katika mdomo ambao risasi hupitia kwenye bunduki iliyokuwa jirani na shingo yake.
“Sina pesa mimi jamani ni mwanafunzi…..mimi mwanafunzi jamani…” alijitetea wakati huo Joy yeye yupo kimya. Jibu hilo lilikuwa karaha kwa watu hawa wabaya, waliendelea kumpiga Michael kwa awamu huku kwa maksudi wakiwa wameifungulia luninga iliyokuwa hapo ndani sauti ya juu hivyo mtu wa nje hakuweza kusikia kinachoendelea. Kadri jinsi Michael alivyojitetea ndivyo majambazi hawa walianza kupatwa na wasiwasi huenda wanamuhukumu mtu ambaye si sahihi
“Kocha….una uhakika ni chumba namba 18……mbona humu tumekuta mwanafunzi!!!.....” Mawasiliano hayo kidogo yakafufua ndoto za Michael na Joy kupona dhidi ya watu hawa.

****
Jitihada za Joyce Keto jijini Dar es salaam kumpata Michael hazikuzaa matunda, pale nyumbani alipokuwa akiishi Michael walidai kuwa aliondoka ghafla na hawafahamu alipo japo si mara ya kwanza kufanya hivyo. Rafiki zake Michael walimuelezea kwamba alikuwa katika hali ya unyonge sana kabla ya kutoweka bila kuaga. Majibu hayo yalimtia mashaka sana Joyce, aliogopa sana kuwaambia watu ukweli juu ya nini kilichotokea walipoonana na Michael kwa mara ya mwisho.
Michael alikuwa amemfumania akiwa na mwanaume mwingine!! Hilo ndilo jambo aliloamini kuwa limesababisha kutoweka kwa Michael katika mazingira ya kutatanisha.
“Lakini mimi sikuwahi kuwa na uhusiano na Michael licha ya watu wengi sana kuhisi mimi na yeye ni wapenzi.” aliwaza na kuwazua Joyce Keto. Ina maana alichukulia serious watu walipotuita wapendanao!! Alijiuliza. Aliogopa sana kumshirikisha mtu yeyote juu ya uhusiano wa kutoweka kwa Michael na tukio la kufumaniwa kwake. Kichwa kilimuuma sana kila alipojaribu kumpigia simu Michael na kuendelea kupata jibu lile lile kwamba namba anayopiga haipatikani.
“Kama amejiua je???.” ghafla wazo hilo liliiteka akili ya Joyce. Mh!! Mtihani!! Alihitimisha mawazo yake kwa kupanda gari na kuelekea chuoni, foleni kubwa barabarani ilimtia hasira. “ah!! Elfu tatu kitu gani bwana.” alijisemea huku akiomba kushuka kisha akakwea bajaji, ghadhabu yake ikapungua kidogo kutokana na kupata hewa ya kutosha. Dakika kadhaa zilitoweka Bajaji ikawasili katika viunga vya chuo. Joyce akashuka na kulipa pesa, kisha hatua kwa hatua akajikongoja taratibu hadi mbele ya ofisi alizokuwa amepanga kwenda.
“Nimejaza namba ya simu ambayo si sahihi!!.” alijieleza Joyce mbele ya mkuu wa kitengo hicho.
“Bwana eeh!! Mmezidi na nyie haya chukua uangalie mwenyewe wino wa kufutia huo hapo utajirekebishia, yaani watu wazima tunakuwa kama shule ya chekechea ah!!!” alizungumza kwa hasira mwanamke aliyekuwa katika kitengo hicho. Kwa Joyce huo ulikuwa ushindi mkubwa sana, ni jambo lililompeleka.
“Huku wasichana huko wavulana” maelezo tosha kabisa kwa Joyce. Haraka haraka alianza kupekua katika majina ya wanaume 1…2….3….4….5…..alizihesabu namba hadi akafikia thelathini na tatu ‘Michael Msombe’!! moyo ulimpasuka na kumuongezea hamu ya kujua kilichoandikwa mbele yake, Mugumu Serengeti!! Ndio wapi sasa huku!!! Alijiuliza Joyce huku akirudia mara mbilimbili kulisoma jina hilo bila dalili yoyote ya kuliweka akilini mwake ipasavyo.
Mkoa wa Mara!! Msamiati mwingine tena. Ili kuhifadhi kumbukumbu hiyo aliamua kuitumia simu yake kuandika kila alichoona ni kigumu kumeza kwa haraka haraka.
“Michael ameenda wapi huku…hivi ni Tanzania…” alijiuliza Joyce.
“Hivi wewe, mbona mzembe hivyo humalizi tu!! Unaboa bwana.” alilaumu yule mama aliyempa Joyce faili kwa ajili ya kufanya marekebisho.
“Ah!! Samahani na ikiwa unataka kuhamishwa sehemu ya kufanya field unafuata process gani???” badala ya kujibu aliuliza swali jingine Joyce na kumtia hasira yule mama.
“Hebu nipishe hapa ushanitia hasira….toka toka toka…tafadhali!” Joyce hakutaka shari huyoo akajiondokea, aliona nyumbani ni mbali sana akiwa ndani ya daladala alifungua simu yake katika sehemu ya internet akaenda google kisha akatafuta google map na kuandika Mugumu Serengeti, ilichukua sekunde kadhaa kutoa jawabu kwamba haikufanikiwa kupakua (load).
Simu ya Joy haikuwa na salio la kutosha. Kompyuta yake ndogo nyumbani ilitumia sekunde chache ikaleta majibu ya kuridhisha.
“Michael ndo ameenda huku kweli ama amelaghai pale ili nisifahamu alipoelekea??” kabla hajapata jawabu simu yake ya mkononi iliita, ilikuwa namba mpya kwake.
“Haloo!!.” aliita

Monday, September 17, 2012

HATIA---03


Na George Iron


“Binti!!!...binti!!!! we dada….” Aliita huku akijaribu kumtikisa kidogokidogo, hakupata jawabu lolote lile. Funda la hasira likitiwa hamasa na uoga aliokuwa nao lilimkaba na kujikuta akijuta kumsaidia yule binti kulipa nauli na kujitambulisha mbele za watu kwamba anafahamiana naye. Uvumilivu ukamshinda mtoto wa kiume akajikuta anamwaga chozi, ilianzia hasira kumkaba kooni, mara macho yakawa mekundu, kisha machozi yakatoka halafu kikafuatia kilio cha kwikwi. Michael alilia sana kwa mtihani mkubwa uliokuwa mbele yake hakuelewa ni vipi anapata suluhu kwa sasa.
“Kaka…..kaka…..” sauti ya kike ilimshtua Michael kutoka katika kilio kikuu
“Mh!!! Aah!! Binti…..umekuwaje…”
“Nikuulize wewe….aaaaah!!! nimeteleza kutoka bafuni…kichwa kinaniuma jamani ah!” alilalamika kwa uchungu, Michael hakuamini macho yake kwamba binti alikuwa anazungumza huku akiwa amekaa kitako.
“Pole sana pole…..unaweza kusimama????” aliuliza
“Hapana kiuno kinauma sana sidhani kama naweza kusimama” jibu hilo lilirudisha mawazo upya kwa Michael lakini wakati huu hakuumia kama alivyoumia awali. Binti alijivutavuta kwa msaada wa Michael hadi akakaa kitandani kwa kujilaza maana hakuweza kukaa imara.
Baada ya muda binti alipitiwa na usingizi na kumpa fursa Michael kuwaza ni nini atafanya kuepuka hilo janga alilolivaa mwenyewe.
“Kesho sisafiri na huyu binti..wema wangu umetosha sasa, sibadili mawazo tena kama nilisema kuwa NIPO NAYE hilo neno nalifuta rasmi, mimi simjui bana!!!” alijichukulia maamuzi hayo kijana Michael.
Majira ya saa tatu usiku binti alikuwa ameamka tayari kutoka usingizini, kwa upande wa Michael bado alikuwa hajalala kwa sababu ya kuumiza kichwa juu ya uamuzi anaotaka kuuchukua.
“Umeamka??” Aliuliza swali ambalo alilitambua jibu lake
“Eeh!!!”
“Nikuletee chakula gani???”
“Maji kwanza halafu chakula nichagulie”
“Mh!! Wewe chagua bibie wala usiogope sawa eeh!!!” alijibu Michael
“Haya chipsi na mishkaki, tia pilipili, tomato, ukwaju, saladi, chumvi, na nini vile ndimu eeh!!” aliongea haraka haraka kwa utani Michael akajikuta anatoa tabasamu huku akisugua viganja vyake katika mkono wa yule binti. Bila kuaga alitoka nje na kurejea baada ya nusu saa akiwa na chakula na maji, akamsaidia binti aweze kukaa kisha akafungua chakula, kwa akili ya kujiongeza akaanza kumlisha yule binti, kila macho yao yalivyogongana Michael alikuwa wa kwanza kukwepesha, alikuwa ni mwanaume mwenye aibu sana mbele ya wanawake huo ni udhaifu uliokuwa wazi kwake. Walitumia saa moja zima kula chakula hadi kukimaliza, Michael licha ya kumwonea huruma binti lakini azma yake ya kumwacha pale gesti ilikuwa palepale.
“Michael wewe ni mwema sana asante sana kwa wema uliouonyesha kwangu…” sauti nyororo ya binti ilipenyeza katika masikio ya Michael..
“Sijui nikulipe nini lakini ubarikiwe sana, naomba kitu kimoja nikuombe na ninaamini utanielewa.”
“Kitu gani tena.”
“Waonaje kama ukiniacha hapa uendelee na shughuli zako mimi nimekuwa mzigo mkubwa sana kwako angali u kijana mdogo tu, naomba kesho unitoe nje na uniache barabarani hapo heri niwe ombaomba maana ndio maisha niliyoyachagua tofauti na kule nilipokuwa, nia yangu ya kuondoka kule imefanikiwa huo kwangu ni ushindi mkubwa sana…” aliendelea kuzungumza huku akijilazimisha kutabasamu.
Maneno ya yule binti yalimshtua sana Michael kwani alikuwa amepanga kumuacha kinyemela lakini anashangaa binti kwa hiari yake mwenyewe anaomba aachwe.
“Kwa nini unaongea maneno hayo dada yangu, mimi bado sijakuchoka.” alidanganya Michael
“Sijasema umenichoka wewe unadhani utaendelea kuwa namimi hadi lini na wapi???.” Swali hilo lilikuwa gumu sana kwa Michael kwani hakika jibu lake lilikuwa ni muda muafaka wa kumwacha yule binti.
“Usiumie sana kaka Michael….wewe ni mwanaume wa kipekee, Mungu atakulipa katika njia zako utakazoenda nitakukumbuka sana na siku moja utakutana tena na mimi nikiwa salama mimi sitakusahau na hata wewe ukiniona usisite kuniita kwa nguvu zote JOYCEEEEEEEEE!!!!!! Mimi nitageuka”
“Hah!! Kwani unaitwa nani wewe na huyo Joyce ni nani??.” Aliuliza Michael huku akiweka kiuno chake vizuri pale kitandani.
“Ooh!! Ulizoea kuniita binti mwone!! Naitwa Joyce mie” Alizungumza yule binti
“Unaitwa Joyce….we acha utani”
“Utani gani mie Joyce jina langu la kuzaliwa kwani vipi??”
“Kuna msichana mmoja anaitwa Joyce…”
“Vipi wifi yangu nini??.” alidakia Joyce
“Hapana alikuwa rafiki tu ndio maana nilishtuka kumbe na wewe ni Joyce…” alizungumza kwa uchangamfu mkubwa Michael.

Kwa maongezi yao ya usiku uliopita Michael alijikuta akivunja kwa mara nyingine tena makubaliano yake na moyo wake, kwa kuwa Joyce alikuwa na uwezo wa kutembea japo kwa shida sana Michael aliongozana naye kuelekea kituo cha mabasi wakiwa katika teksi iliyowafikisha haraka, Michael akamsaidia Joyce wakapanda ndani ya basi la Mombasa Raha katika siti za mbelembele na safari ya kuelekea Mwanza ikafuata. Ubora wa barabara hiyo ya kuelekea Mwanza ulimpa ahueni Joyce kwani hakutoneshwa kiuno chake.
“Nitakuacha Mwanza sawa.” ndilo neno la muafaka kati ya Joy na Michael waliloamua usiku uliopita. Safari ilionekana fupi sana kwa Michael kwani nafsi ilikuwa haijaridhika kumuacha njia panda Joyce ambaye kwa majina amefanana na binti aliyempenda wakati akiwa jijini Dar es salaam.
Saa tano asubuhi safari ya masaa mawili ilikuwa imefikia kikomo katika stendi ya Nyegezi jijini Mwanza. Si Michael wala Joyce aliyekuwa anaufahamu fika mji huu uliotawaliwa na milima ya hapa na pale hivyo kila mmoja alimtazama mwenzake.
“Tupeleke lodge yoyote iliyopo karibu na iwe nafuu kiasi.” alijieleza Michael kwa sauti ya chini mbele ya dereva.
“Poa..” alijibu dereva kisha Michael na Joyce wakapanda safari ya dakika kumi ikawafikisha mbele ya lodge iliyojulikana kwa jina la DOUBLE G, baada ya kupewa pesa yake akatokomea yule dereva.
“Chumba bei gani???...aah!! kwanza vyumba vipo??” Aliuliza Michael
“Vipo lakini subiri kidogo hebu…we nanii Dory, hivi chumba namba 18 kipo wazi au alilipia kulala yule bwana.” waliulizana wahudumu katika hali ya kunong’ona kisha likapatikana jibu kwamba kilikuwa wazi
“Chumba kipo elfu kumi si mnalala au ni show time kama ni show basi elfu tano!!”
“Hapana tunalala” Alisema Michael huku akitoa pesa mfukoni na kulipia chumba.
Hakuna aliyekuwa amechoshwa na safari lakini kutokana na kila mtu kuwaza la kwake walijikuta wakipitiwa na usingizi kila mmoja kwa wakati wake. Hadi saa moja usiku ndipo mkojo ulimwamsha Joy na yeye akamwamsha Michael.
“He!! Tumelala hivyo…..” Alijiuliza Michael wakati huo tayari Joy alikuwa ameingia msalani.
Aliporejea Michael yeye alikuwa amevaa viatu vyake na alikuwa na kila dalili ya kutaka kutoka.
“Wapi tena ndugu yangu jiji lenyewe hulijui tuachie sisi.” Alitania Joy
“Naenda kucheki benki kama mkopo umeingia si unajua tena…vipi twende wote”
“Mimi sitoki humu ndani usije ukanipoteza bure” alijibu Joy, Michael akajiondokea.
Dakika thelathini baadaye mlango uligongwa.
“Hebu ingia au unadhani umepotea” alijibu Joy na kweli kitasa kikashushwa wakaingia watu watatu waliojazia miili yao. Bunduki ndogo iliyowatangulia mkononi ilitosha kumnyamazisha Joy.

****

Michael alikuwa na furaha ya ajabu sana na alijiona ni mtu mwenye bahati kila mara, ndio alikuwa na bahati! Maana pale benki hapakumkatisha tamaa ila kumwongezea furaha tele, pesa ilikuwa imeingia katika akaunti yake pesa ya mkopo!
“Huyu Joy huyu ana miujiza yake na nikifika lazima nimwambie baraka anazoniletea.” alisema Michael bila watu wengine kujua alikuwa anaongea nini, alipovuka barabara kuelekea upande mwingine akili ilimrudisha tena upande aliokuwa lengo ni kununua hiki na kile kwa sababu ya safari ya kesho yake safari ya kuelekea Mugumu Serengeti, alinunua vitu kadhaa wakati huo akiwa na jeuri ya pesa mfukoni mwake.
“Joy, Joy, Joy…mh!! Ni msichana wa aina yake” alikiri Michael baada ya kufanya tathmini ya Joy akiwa si mgonjwa kama alivyo wakati huo.

Ni mrefu kama mnyarwanda, si mweupe sana lakini weusi wake unatosha kumwona gizani na kwenye mwanga, midomo yake ina majeraha lakini kama ikipona ni mtego tosha kwa mwanaume yeyote asiye na subira, kifua chake ambacho Michael aliweza kukiona bahati mbaya alipokuwa ameanguka kutoka bafuni kilikuwa na mzigo mdogo wa embe dodo ambazo hazikuwa na mpango wa kuanguka katika siku za karibuni, tabasamu lake la nadra liliruhusu vishimo vilivyojificha kuchomoza na kuzidi kuing’arisha nuru ya uso wake. Hiyo ni picha ambayo aliijenga Michael akiwa katika manunuzi ya hapa na pale, mawazo hayo yalimpeleka katika ushawishi, ushawishi nao ukachipua upesi akajikuta anashawishika, kishawishi cha kuondoka na Joy kuelekea Mugumu Serengeti mahali ambapo hajawahi kufika kabla.
“Nitaondoka naye…atapona mbele kwa mbele naamini atafurahi sana” Alisemezana na moyo wake huku akirejea kule alipomwacha Joyce.

* * *

Kaubaridi ka asubuhi asubuhi katika jiji la Mwanza maeneo ya Nyegezi karibu na chuo kikuu cha mtakatifu Augustino kaliwachochea wavutaji wengi wa sigara kununua pakiti kwa pakiti kukabiliana nayo huku wasiokuwa wavutaji wakipekua huku na huku kujua ni wapi waliyaacha masweta yao hapo ni baada ya kuingia hasara ya kununua miamvuli mipya kutokana na mvua iliyonyesha kuanzia alfajiri.
Kijiwe cha Bob Soya cha hapo Nyegezi kona kilikuwa na wadau wengi sana, wachache walikuwa na uwezo wa kununua kete za bangi huku wengi wakisubiri za ‘kugongea’ kwa wenzao. Ushikaji uliwekwa pembeni kutokana na hali halisi ya hewa, kila mmoja alitamani moshi mkali wa madawa hayo uendelee kupenyeza ndani ya mapafu yake kisha kutoka nje kupitia pua na mdomo wake. Pusha aliifurahia sana hali hiyo ya hewa kwani aliuza kwa wingi sana bidhaa zake. Mteja mmoja peke yake ndio alikuwa hazungumzi sana, yeye na bangi, bangi na yeye huku muda ukisogea.
Matusi makali makali yalizunguka eneo hilo ambalo lilikuwa jirani na nyumba ya kuishi watu. Matusi hayo mwishowe yakavunja amani iliyotawala kwa muda mrefu na kuzaa vita ndogo iliyosababishwa na ukosefu wa ustaarabu wa bwana mmoja aliyelazimisha kupewa kipisi cha bangi kwa ulazima huku akiwa hana pesa ya kukidhi hiyo haja yake. Ubabe wake uliwatetemesha wengi lakini leo alikuwa amempata kiboko yake.
“Mkishagombana ndio mtapata zawadi ya ‘ndumu’ ama!!!” alizungumza yule mzee ambaye alikuwa kimya muda wote akivuta bangi kistaarabu. Wote waligeuka kumwangalia kwa sekunde kadhaa kisha wakataka kumpuuza na kuendelea kushabikia ugomvi.
“Kaka, hebu wapatie idadi wanayotaka nitalipia” aliongea kwa jeuri akimtazama yule muuzaji. Amri hiyo ilipunguza makali ya ugomvi na kuuvunja kabisa, maadui wakawa marafiki na hasira kuwa vicheko. Huyu alikuwa ni mzee Robert Chacha, mfanyabiashara maarufu wa samaki katika jiji la Mwanza ambaye kutokana na kabila lake la kikurya isitoshe alikuwa mwanajeshi mstaafu alitokea kuwa maarufu kwa jina la ‘poti’. Ilikuwa mara yake ya kwanza kukifikia kijiwe hichi cha Bob Soya na hakuna aliyemtambua zaidi ya kujua kuwa ni mvuta bangi wa kawaida aliyezidiwa na baridi.

Ndio Poti alikuwa amezidiwa na baridi hilo halikuwa na ubishi, lakini jeuri yake ya kukivutisha kijiwe kizima ndio ilimshtua kila mtu.
“Shilingi ngapi jumla??” aliuliza Poti baada ya kila mmoja kuwa ameridhika na pia mzigo kumwishia muuzaji. Muuzaji alimtajia bei kwa uoga akidhani huenda ni bangi zilikuwa zimemchanganya huyu mzee na kujikuta anazungumza vitu asivyovijua lakini haikuwa hivyo, Poti alizama katika kibegi kidogo alichokuwanacho akakipekua kwa kubahatisha akachomoka na noti kadhaa zilizotosha kutibu njaa ya muuza.
“Hiyo nyingine tunza…” alikataa kupokea chenchi aliyorudishiwa, akafunga kibegi chake na kutoweka.
Alipoondoka nyuma aliacha gumzo huku kijiwe kikiwa kimesahau kuhusu ugomvi uliotaka kuibuka. Safari ya Poti ilikuwa haina uelekeo maalum ndio maana alijikuta akiishia katika nyumba ya kulala wageni ambayo alienda kwa minajiri ya kubadili nguo zake zilizolowana lakini kama bahati mbaya na nzuri kwake akamkuta msichana asiyekuwa na uelekeo ni huyo aliyemsindikiza chumbani kwenda kuwa jalala kwa muda, yaani kuuchukua uchafu wa Poti na kuuhifadhi.

Poti alipofika ndani aligundua hiyo haikuwa tabia yake labda huenda ni bangi aliyovuta imemchanganya, badala ya kumtumia yule msichana aliyetegemea ujira baada ya kazi alimshangaza alipomlipa na kumruhusu kuondoka. Baada ya yule changudoa kuondoka Poti alibadili nguo zake na kupitia mlango wa nyuma akatokomea.

Hicho kilikuwa chumba namba 18, chumba ambacho Michael na Joyce wake walikuwa wamekilipia kwa ajili ya hifadhi ya usiku mmoja bila kujua kama kilitumika siku hiyo hiyo.

TATIZO

Mdomo wa bunduki uliokuwa umemuelekea Joy pale kitandani haukuwa umekosea njia hata kidogo, walikuwa ni walewale wavuta bangi waliopewa ofa ya kuvuta bure, tayari walikuwa wameusahau wema wa Poti kuwatoa katika baridi bila gharama yoyote sasa wanataka kujua ana nini katika begi wakiamini ni halali yao, ama kweli kijiweni hakuna rafiki wa kweli!!. Poti hakuwa pale ndani tena, walikuwepo watu wasiokuwa na hatia yoyote.
“We Malaya yuko wapi bwana yako????” sauti nzito ilimuuliza Joy pale kitandani wakati huo alikuwa anatetemeka na kuyasahau maumivu yaliyokuwa yanamkabili.
“Sina….bwaaa..na!!!.” alijibu kwa kutetemeka sana Joyce. Kitako kimoja tu cha nguvu cha bunduki kiliiweka akili yake sawa
“Bwana yako yuko wapi malaya wewe!!!.” sauti hii ilikuwa kali kuliko ya kwanza Joy hakutaka kuleta ubishi.
“Ametoka kidogo….atarudi” alilazimika kujibu kwa hofu ya mtutu wa bunduki.
“Soya….tumsubirie…..atarudi huyo fala muda si mrefu..” walinong’onezana wao kwa wao, wakati huu walikuwa wameutoa ule mtutu wa bunduki jirani na Joyce lakini alikuwa anatetemeka sana. Baada ya dakika kumi zilisikika hatua zikijongea katika mlango wa chumba namba 18. Majambazi watatu walijibanza nyuma ya mlango huku mmoja akiingia uvunguni mwa kitanda. Mlango ukarudishiwa kidogo.
“Surpriiiiise!!!!!!!!” ukelele ulisikika kutokea nje ya mlango, ilikuwa sauti ya Michael ni Joy pekee aliyeitambua, moyo wake ukakata tamaa, alijua Michael alisubiri ajibu chochote. Laiti kama angejua kilichopo hapa ndani wallah!! Asingethubutu kuingia! Alijisemea Joyce huku Michael akiendelea kupiga kelele pale nje.
Joy hakujibu chochote kile kwani alikuwa na hofu juu ya wale watu wabaya waliokuwa chumbani hapo. Sura zao hazikuwa na mzaha hata kidogo walimaanisha walichokuwa wamekifuata hapo ndani. Taratiibu mlango ukaanza kufunguliwa kwa mguu kumaanisha kwamba kuna kitu mikono ilikuwa imebebwa hivyo kushindwa kutimiza wajibu huo.
Uso wa Michael ulikuwa umechanua kwa tabasamu murua, hakuwa amevaa zile nguo alizotokanazo nje. Wakati huu sasa aliweza kuyaonyesha maungo yake vyema, kifua kilichogawanyika katikati kutokana na mazoezi ya hapa na pale kilichomoza katika fulana iliyokuwa imembana hasa, suruali aina ya jinsi ilimchora miguu yake ilivyokuwa imara bila kuyumbishwa na matege ya aina yoyote kilikosekana kitu kimoja tu kukamilisha utanashati wa Michael, hakuwa akitabasamu! Ndio na hakupaswa kufanya hivyo maana Joy alikuwa ameyatumbua macho yake na kutokwa jasho kitu kibaya kilikuwa kimemtokea!! Taratibu bila kuzungumza chochote Michael ambaye alikuwa amesimama sasa mbele ya chumba hicho kimoja naye alimkazia macho Joy. Michael hakupaswa kusubiri kuambiwa akae chini, pigo moja tu katika mbavu zake lilimfanya ajikunje huku akitoa ukelele mdogo, akili ilikataa asikae chini lakini mwili bila ubishi ulilainika hatimaye akasalimu amri mbele ya Joy, mtutu wa bunduki ukafuata katika shingo yake, hofu ikaanza kutanda hofu ikamtawala na uoga.

ITAENDELEA















Friday, September 14, 2012

HATIA --- 02

Na GEORGE IRON


         Hospitali ya mkoa wa Shinyanga kwa ujumla haikuwa mbali sana kutoka mahali basi hilo la Najimunisa lilipopatia hiyo tafrani, kwa maamuzi yaliyoafikiwa na kila abiria yule binti walimzoazoa kutoka pale chini na kumweka katika siti ya mbele ambayo ilikuwa na uwezo wa kupokea watu watatu, hakuwa akitokwa na damu lakini alikuwa akigumia kwa sauti ya chini sana, mwanamke mmoja alikaa pamoja naye kwa ajili ya kumsaidia huku Michael naye akiwa karibu yake.

                                                      ******

       Hospitali ya mkoa wa Shinyanga ndio kwanza ilikuwa katika mgomo wa madaktari wakitaka mwenzao aliyewekewa zengwe na kufukuzwa kazi baada ya kushindwa kuokoa maisha ya mtoto wa Kigogo arejeshwe kazini hivyo hakuna huduma zilizokuwa zikitolewa pale licha ya madaktari kuwepo eneo hilo la Hospitali mjini Shinyanga. Kundi la wanaume wanne wakiwa wamembeba mgonjwa wao liliingia kwa uharaka wa kuhitaji huduma pale ndani, hakuna yeyote aliyewakaribisha zaidi ya ukarimu walioupata kwa mlinzi pale mlangoni huku akiwaonea huruma, kila mtu alikuwa bize sana na mambo yake binafsi yasiyoendana na mandhari ya hospitali.
“Nesi nesi…” mwanamme moja aliita lakini alijibiwa kwa jicho kali kisha mwanamama huyo akatoweka. Kwa ujasiri waliamua kujitafutia wodi mojawapo na kumlaza yule binti kitandani kisha wakaanza kuhaha kuwatafuta madaktari ambao hata hawakuonyesha kujali. Mwanzoni walikuwa wanaume wanne pamoja na mwanadada asiyejitambua hata kidogo akiwa katika maumivu makali sana ambayo hakuhitaji kujieleza mwenyewe bali jinsi alivyokuwa ameuma meno na kuikunja sura yake lilikuwa jibu tosha, baada ya muda wakabaki watatu, wawili na hatimaye mmoja Michael!! Ndio alikuwa Michael peke yake pamoja na binti.
             Nafsi ya Michael ikaingia katika mgogoro mkali, mgogoro binafsi, maamuzi yalikuwa mengi lakini hakujua lipi ni sahihi. Akiwa katika wimbi la mawazo alisikia anaguswa begani.
“Aah!! Kijana nimekutafuta kweli, ni zaidi ya saa zima sasa nilikuwa napita hapa lakini sijui kwa nini hii wodi nilikuwa naivuka.” sauti nzito kutokana na umri kwenda ilimweleza Michael ambaye alibaki kuduwaa ilikuwa mara yake ya kwanza kufika katika mkoa huu uliotawaliwa na jamii ya wasukuma halafu anatokea mtu anamfahamu.
“Mimi?.”
“Ndio wewe!!!.”
“Aaah!!! Eheee.” aliuliza Michael ili apate kujua shida ya yule mtu.
“Unawahi kusahau wewe, mimi ni yule mlinzi wa pale getini mwanangu poleni sana baba!!!! Pole sana” alijieleza yule mlinzi. Michael hakuwa na kumbukumbu kabisa kwamba pale kwenye basi walipofikia muafaka wa kumwahisha binti hospitali watu walichangachanga walichonacho na kufikisha shilingi laki mbili na nusu ambayo walimkabidhi, alipozipokea mkononi ndivyo hivyo hivyo alizishika hadi waliposhuka na kumfikia mlinzi wa geti, wakati anaandika jina lake katika kitabu cha orodha ya wageni ndio wakati huo huo aliziachia zile pesa na kuzisahau, jambo jema mlinzi huyu aliyejitambulisha kama mzee Matata aliona tukio hilo na kuokoa pesa za Michael na sasa alikuwa amempata kwa ajili ya kumpatia.
Michael alishangazwa na uaminifu aliokuwa nao babu huyu wa makamo mrefu, mwenye mwili uliojengeka na ndevu zake zilizokuwa na mvi kiasi,
“Kwa nini amenirejeshea hizi pesa??.” Alijiuliza Michael
“Asante sana mzee wangu asante sana.” Michael alijaribu kumpatia kiasi fulani cha pesa lakini mzee Matata alikataa kabisa huku akimwonea huruma Michael kwa hali aliyokuwa nayo.
“Ngoja niangalie kama utapata huduma walau ya kwanza maana huyu nani vile anaitwa??.”
“Aaah!!! Mhh!! Huyu?? Anaitwa nanii Mariam eeh!!! Mariam.” alijibu Michael kwa kujiumauma
Mzee Matata alipotoka Michael naye alifikiria kuondoka na kumwacha binti peke yake, akili ilikuwa imemruhusu lakini wakati anapiga hatua mlangoni aliisikia nafsi yake ikimtamkia neno ‘NIKO NAYE’ ambalo alilitaja pale ndani ya basi, nafsi pia ilimsuta kwa pesa aliyorejeshewa na mzee Matata, kwa kutoroka ilimaanisha kwamba amefanya dhulumati na kuweka maisha ya binti katika hatihati. Michael alizishusha pumzi zake kisha akarejea tena pale wodini kusubiria harakati za mzee Matata kama zitazaa matunda.

                                    ******
  
Akiwa ni mtoto wa tatu wa mzee Akwino Msombe ni yeye pekee aliyejaaliwa kielimu hadi hapo alipofikia, jina Michael Msombe lilikuwa maarufu sana katika shule ya sekondari Musoma Technical alipomalizia kidato cha nne kutokana na umahiri wake katika kucheza mpira wa miguu, jina hilo likaendelea kupeta katika shule za Mara Secondary na baadaye Minaki kutokana na ubora wa Michael katika suala zima la uhamasishaji wa maendeleo na kuwa mshauri bora kwa wenzake hasahasa baada ya kufanya jitihada kubwa na kuunda tawi la FEMA katika shule yake.
Katika chuo kikuu cha Dar es salaam Michael hakuwa akicheza mpira tena lakini aliendelea kuhamasisha hapa na pale lakini athari kubwa iliyopunguza uwezo wake wa kutimiza wajibu ilikuwa ni jinsia ya kike ambayo kwa mara ya kwanza alikuwa nayo karibu zaidi ya awali alipokuwa katika shule za wanaume watupu. Wasichana hawakuchelewa kutambua kitu fulani katika mwili wake, kijana aliyecheza mpira kwa kujituma miaka kadhaa iliyopita mwili wake ukiwa umejengeka vyema, mrefu wa wastani na rangi yake maji ya kunde ilimfanya aonekane mtanashati pindi anapochomekea shati lake la mikono mirefu katika suruali yake iliyopigwa pasi vyema, anapovaa jeans na fulana yake bado alionekana nadhifu, na hakuharibikia siku aliyojisikia kuvaa pensi kwani mguu wake ulistahili kuonwa na watoto wa kike.
Hayo yote yalisindikizwa na jicho hadimu sana ambalo likimtazama mwanamke atajiuliza mara mbilimbili Michael anamaanisha nini?? Maskini Michael wa watu hakuyajua hayo yeye alikuwa akihisi huenda kizuri katika mwili wake ni kishimo kidogo (dimple) katika shavu lake la kuume jambo alilojitambia tangu utotoni.
                    Akiwa na miaka 24 tu aliingia katika msukosuko wa kimapenzi wasichana wengi walimtamkia kwa midomo yao kuwa anawatesa lakini alichukulia ni utani hadi siku moja na yeye alipogundua kwamba anateswa. Ni siku ambayo alikutana na Joyce msichana ambaye walicheza naye utotoni na kisha kusoma wote shule ya msingi baada ya kumaliza shule ndipo rasmi wakapotezana baada ya Michael kuchaguliwa kujiunga Musoma tech kwa ajili ya kuendelea na kidato cha kwanza huku Joyce yeye akienda Nganza sekondari Mwanza.
Hapo chuoni walikutana mgahawani wakati Michael ananawa na Joyce anatafuta meza ya kukaa, ilikuwa ni furaha ya hali ya juu ambayo iliunda upya urafiki wao wa utoto na kuufanya wa ukubwani, kwa Joyce ilionekana kama imetosha lakini kwa Michael alitaka zaidi ya pale jambo lililomvuruga sana akili yake. Siku ya kuzaliwa kwake alitamani ibadilike kwani bila hivyo angeendelea kuumia miaka nenda miaka rudi.
“Kwanini Joy amenitenda hivi??.” alijiuliza kila siku.


                                         *****

Monday, September 10, 2012

HATIA--- 01

          Na  George Iron ( Ubunifu Wetu)

               Safari nzima hakutaka kuzungumza na mtu yeyote hivyo alikuwa amepachika ‘earphone’ masikioni mwake ili hata asiweze kusikiliza watu walikuwa wanazungumza nini mara chache sana alipata nafasi ya kusikia mawili matatu hasahasa pale wimbo ulipokuwa unaisha na kuachia nafasi ya wimbo mwingine kuingia, katika kibegi chake kidogo alikuwa na takribani betri nne zilizokuwa zimechajiwa usiku uliopita ili asipatwe na usumbufu wa kuzimikiwa simu katika safari yake hiyo ndefu kiasi ya kuelekea wilayani Serengeti mkoa wa Mara. “Hivi wazazi wangu ni wendawazimu…sas a waliniita Michael ili iweje kwa nini hawakuniita hata Masumbuko???.” Alijiuliza kijana huyu mrefu wa wastani ambaye umbo lake kwa kumtazama ungemkadiria kuwa na miaka ipatayo thelathini lakini kiukweli ndio kwanza siku tatu zilizopita alikuwa ametoka kusheherekea kutimiza miaka ishirini na tano siku ambayo ilianza vizuri sana asubuhi kwa kupokea jumbe tofautitofauti kutoka kwa ndugu jamaa na marafiki waliokuwa wanaikumbuka tarehe hiyo.

            Karibia kila mmoja alimtakia heri na fanaka katika maisha yake, huku wakikumbuka pia kumtakia aishi miaka mingi. “Joyce atakuwa ameisahau hii siku au kuna tatizo jingine??.” Michael alijiuliza baada ya kutouona ujumbe wake kati ya jumbe zote alizopokea. Kwa kuwa Joyce hakuwa akikaa mbali sana na mtaa anaoishi Michael jijini Dar es salaam, basi Michael alitumia fursa hii kwenda kumpa surprise rafiki yake huyo wa kike tangu utotoni japo hawakuwahi kuvuka urafiki na kuwa wapenzi lakini ndipo walikuwa wanaelekea. Michael alikuwa anatabasamu njia nzima, kwani aliamini kuwa ile hali tu ya kumkumbusha Joyce tukio hili ni lazima atamrukia na kumkumbatia, kitendo ambacho kwa Michael ni zaidi ya zawadi, lile joto la kipekee la binti huyo lingeweza kumchangamsha na kujisikia kweli amezaliwa siku hiyo.                
              
Utajuaje, huenda pia atanibusu?? Alijisemea Michael kisha akafanya kicheko kidogo cha kujilazimisha. Kisha akatikisa kichwa kama vile kuna jambo alikuwa analikataa. Sasa alikuwa ameufikia mlango. Akalazimika kunyata ili amshtue Joyce, na hatimaye apokee lile kumbatizi maridhawa. Alichokikuta Michael nyumbani kwa akina Joyce ndicho kilibadili ghafla mipango yake ya kufanyia mazoezi ya vitendo (field) katika jiji la Dar es salaam na kuamua kuelekea mji mdogo wa Mugumu Serengeti mkoa wa Mara bila kutarajia. Hakujua kwa nini ameuchagua mji huo lakini alijikuta katika maamuzi hayo. “Lakini kwani nilikuwa nimemtamkia kuwa nampenda?...mim i ni mpuuzi huenda labda ndio maana hakushtuka nilipomkuta.” Alijiuliza Michael huku akijaribu kunywa maji ili kulegeza donge la hasira lililokuwa limemkaba kooni . “Hivi ninachokasirika ni nini hasa wakati hajui kama nilikuwa namtaka?...ah!! huu ni upuuzi hakika.” Alijiliwaza Michael huku akishindwa kuyanywa yale maji na kuyafunika kisha kuendelea kupata burudani ya muziki baada ya muda alipitiwa na usingizi alikuja kushtuka baada ya mwanamama aliyekuwa pembeni yake kumlaumu kuwa alikuwa anamlalia kila anaposinzia. “Unasema??.” Aliuliza kwa sauti ya juu Michael baada ya kuwa ameathiriwa na sauti kali ya muziki masikioni. “Unanilalia bwana!!!.” “Ah!! Samahani…” Wakati huu alikuwa ameondoa ‘earphone’ masikioni mwake.
                 
                   Safari ilikuwa inaendelea, safari ya kutoka jijini Dar es salaam kuelekea Mwanza kisha mkoa wa Mara. Hii ndio ilikuwa mipango yake. Mipango ya kukimbia maumivu. Baada ya kuomba radhi alitaka kurejesha tena earphone masikioni lakini alisita kidogo baada ya kuvutiwa na vurumai iliyokuwa inaendelea kati ya makondakta wa hilo basi na mwanadada, kisa kilikuwa ni kukosa nauli kwa huyo dada huku akidai kuna mtu anamlipia yuko nyuma. “We mbona unasema kuwa kuna mtu analipa na sisi hatumuoni… nenda ukamguse basi mwambie alipe, yaani wewe umepandia njiani halafu unasema kuna mtu anakulipia, acha kutuzingua basi na ujanja wa kizamani.” Kondakta mmoja alibwatuka kwa ghadhabu akionyesha dhahiri kukerwa na maneno ya yule dada aliyekuwa hajakaa kisafari ndefu kabisa. “Ebwana anayemlipia huyu dada yuko wapi?? Sisi tunamshusha hivyo.” alitangaza kondakta lakini hakuna aliyejitokeza kubeba mzigo huo. “Mi sishukiiiii…sis huki, niacheni, niache hukooo, sitaki kushukaa.” Alilia yule dada kwa sauti ya juu huku akiwa ameng’ang’ania mkono wa yule kondakta hapo ni baada ya gari kuwa limesimama ili ashushwe. Kila mtu alikuwa na shughuli zake hakuna aliyejishughuli sha na sakata hili kwa asilimia kubwa. Waliojaribu kujishughulisha walikuwa wakitabasamu ama kucheka huku wengine wakiongea sauti za chinichini. Haikujulikana wapo upande upi.
                               Michael alikuwa bado anaangalia hilo vurumai linavyoendelea, kitendo cha huyo dada kilimkumbusha adha ya usafiri katika jiji alilokuwa ametoka la Dar es salaam lakini kikubwa zaidi ni umasikini unaotawala sehemu kubwa ya Tanzania, lakini kilichomuumiza ni unyanyasaji wa wanawake katika jamii jambo ambalo alikuwa analipinga na hadi kufikia kusomea masuala ya sheria na haki za binadamu akiwa mwaka wa pili katika chuo kikuu cha Dar es salaam na sasa alikuwa anaelekea katika field. Alikumbuka jinsi alivyokuwa anajisikia vibaya iwapo mzee wake anatokea kumnyanyasa mama yake. Ile hali ikajirudia tena baada ya sakata hili. Moyo ukamuuma!!! “Nipo naye huyo!!!.” Alitamka kwa sauti kuu Michael. Hakujua maneno haya aliyatoa wapi lakini aliyatamka kiufasaha na kusikiwa na kila abiria ndani ya basi hilo la Najimunisa wakati huo tayari tairi sita za basi hilo zilikuwa katika ardhi ya Dodoma. Watu wote waligeuka kumtazama kwa mshangao huku kondakta akitaharuki na uso wake haukutabasamu bali ulipambwa na ndita zilizomaanisha hasira. “Sasa muda wote huo ulikuwa wapi kujibu mbona mnaleta ujanja wa kishamba hapa..sasa ulitegemea nitamuacha huyu malaya wako asafiri bure au, acha hizo jombaaa!! Mbona tunatafutiana sababu za kutukana halafu mwishowe mnasema makonda wana matusi.” Kondakta ambaye kimabavu alimzidi Michael alitoa karipio. “Nauli ni shilingi ngapi??.” Badala ya kujibu lawama za yule Kondakta Michael kwa kujiamini kabisa aliuliza swali bila wasiwasi. Ilikuwa ni kama hakumsikia kipindi anabwatuka. “Sio ishu hizo kaka…nigei elfu ishirini na tisa hiyo.” Alijibiwa kwa jazba. Taratibu alijipekua na kutoa noti tatu za elfu kumi kumi akampatia akarudishiwa elfu moja. “Kakae kule nyuma na jamaa yako nafasi inatosha ile pale.” Alielekezwa yule binti ambaye bado machozi yalikuwa yanamtiririka mashavuni na kudondoka chini.
                      
                      Kwa kusuasua alienda na kujibanabana pembeni ya Michael wakati huo gari zima lilikuwa linaitazama filamu hii tamu ya kusisimua. Binti alipofika pale tayari Michael alikuwa amerejesha ‘earphone’ masikioni mwake na wala hakumjibu alipotoa shukrani ya msaada huo. “Mh!! Wanaume wanajua kutesa wanawake da!! Sasa hapo wamegombana nyumbani anauleta ugomvi wao kwenye usafiri ah!!! Ujinga kweli huu.” Alisikika abiria mmoja mwanamke wa makamo akilalamika lawama ambazo hazikupenya katika masikio ya Michael. “Pole dadangu!!!.” mwanaume mwingine upande wa kulia alimwambia yule binti naye akamjibu kwa kichwa. Michael hakuwa na habari kabisa, japo aliamini kuwa mengi tu yalikuwa yanazungumzwa juu yake.

Recent Posts